Ni ujumbe kutoka kwa mdau wa afya, unajieleza! Tafadhali tuachane na kuuliza "nani mjumbe" tukazie "nini ujumbe"! It is very possible that, private practice in India is driven by pay back system, you refer a patient to Apollo you get paid. I just don't have evidence but I am sure move za hospitali kukusanya wagonjwa na kuwapeleka India zitakuwa driven by this payment system, I bet our officials may also be involved. And these people are serious about that business, Apollo wanaanza kuwapa huduma wagonjwa Dubai, so from the airport you start getting services. And the practice is made in such a way unafanyiwa vipimo vingi kadiri inavyowezekana, including those you don't need, the aim being to maximize the cost. I am posted at Christian Medical College Hospital in India, this is a hospital which is not business oriented, but it is the best cardiology centre in India, it is one of the best nephrology centre in India also, iko Tamil Nadu km 120 kutoka Chennai. The cost of services here is 1/3 ya gharama za Apollo and the like, the cost is even cheaper as compared to cost of some services in Nairobi (kuna mgonjwa alikuwa na leukemia Nairobi, gharama ya matibabu Nairobi ilitosha kulipia usafiri, matibabu gharama za kuishi hapa Vellore na akabaki na change), but guess what, no one is referring patient to CMC even in India itself because this hospital does not entertain the system of pay back!!!!! It is very sad in deed! YATOKANAYO...Upo msemo mmoja ulivuma siku chache zilizopita, unasema, "ukiona manyoya, basi ujue keshaliwa" Kwa hivyo, ujumbe huu unaweza ukawa umetufungua macho wengine tuliokuwa tukikuna vichwa kujiluliza kulikoni? Vipi "kutiririka" kwenda India kwa matibabu kwa viongozi wetu kunashamiri na kushika kasi hivi? Mimi kwa mfano nilijiuliza: Je! Hii inatokana na wagonjwa hao kukosa imani na tiba toka kwa wataalamu wetu? Kwamba, wanahisi wanapewa tiba isiyo na kiwango? Au ni imani ya kasumba ya kujitakia au kufuata mkumbo tu kwamba matibabu ya "mzungu" au "mhindi" ama "mchina" yanaponesha vyema na haraka zaidi kuliko yale ya "mbantu" mwenzetu? Hatuamini wala kuuthamini utaalamu wa wataalamu wetu? Ikiwa madai yao kwamba wanakwepa huduma hafifu na mbovu, je, hawa viongozi wanaokuwa wepesi kutaka matibabu nje ya nchi, wanakosaje akili ya kuwawezesha wataalamu wetu kwa vifaa na mazingira bora ya kazi kwa kutumia fedha hizo hizo wanazozipeleka "India" ili nasi Watanzania tujivunie Watalaalamu wetu, wananchi wa kipato cha chini nao wasioweza kwenda "India" nao wapate nafuu ya tiba nzuri? Mbona tunadharauliana hivi? Umewahi kujiuliza ni kwa nini Watanzania wengi wanaohama nchi na kuajiriwa nchi nyingine wanasifika kwa uchapa kazi wao lakini wakiwa Tanzania walidharauliwa hata pale waliposhauri yaliyo ya haki? Ama ndiyo "Nabii hakubaliki kwao?" Fedha wanazolipwa viongozi wetu hawa si zinatokana na kodi za wananchi na rasilimali za mumu humu ndani jamani? Sasa badala ya kuzizungusha humu ndani, ni kwa nini zinapelekwa kunufaisha mataifa ya nje? Ama yote hayo hayana maana kwa kuwa fedha zenyewe, haziendi "nje" kweli bali zinazunguka na kurudi mifukoni mwao? Hii nchi hii, ukisikia "pa" ujue ndiyo hivyo tena...! 3 Comments Na F. Mghanga, tanzmed.com Ni Jumatatu asubuhi. Hali ya hewa ya joto la kadiri ilikuwa ni kitu cha kawaida kwa maeneo haya ya Dar es Salaam kipindi cha miezi hii ya mwisho wa mwaka. Tupo darasani kwenye presentation ya somo linalohusu magonjwa ya figo. Mada ilihusu kushindwa kufanya kazi ghafla kwa figo au Acute Renal Failure kwa lugha ya wenzetu. Lilikuwa somo refu lililozungumzia kwa undani tatizo hilo. Baada ya mwenzetu mwasilishaji kumaliza kuwasilisha somo lake kikafuata kipindi cha maswali na majibu na masomo zaidi kutoka kwa Profesa aliyekuwa anasimamia ile mada. Mada ilikuwa moto. Maswali yetu pamoja na uzoefu wa yule profesa ulitosha kuibua somo na majibu yaliyotosheleza kiu zetu za kujifunza zaidi. Kisha baada ya somo akauliza swali kwa hali ya utani kidogo, nani kati yenu anapenda kuwa Nephrologist (daktari bingwa wa magonjwa ya figo). Wote tulibaki kimya tukitazamana kisha mwanafunzi muwasilisha mada huku akitabasamu alininyoshea kidole akasema "Fabby huyo." Profesa aliniangalia kisha akainamisha kichwa chini kwa masikitiko akasema “I feel sorry for you my friend (nakuonea huruma rafiki yangu)”. Sikuelewa kwanini alisema vile nikashtukia tu namuuliza “why Professor?” Huku bado akiendelea kunitazama akanijibu “because you will be seeing your patients dying everyday”. Jibu lake ghafla likanirudisha nyuma kama mwaka mmoja hivi nikiwa nafanya kazi hospitali moja ya Mission iliyopo mkoa fulani kusini mwa nchi. Ilikuwa siku ya Jumatano asubuhi. Hali ya kaubaridi baridi iliyokuwepo siku hiyo iliashiria kuanza kwa siku njema. Ninaingia wodini na kusalimiana na wauguzi wa wodi yangu kabla ya kuingia ofisini kujiandaa na round. Nilikuwa na kawaida ya kuanza siku kwa kufanya round kwa wagonjwa waliolazwa kabla ya kuingia ofisini kuwaona wagonjwa wengine wapya na wale wanaokuja kwa ajili ya follow up. Baada ya kuwaona wagonjwa kadhaa, nikakifikia kitanda cha mgonjwa mpya aliyekuwa amelazwa usiku wa kuamkia siku hiyo na kuonwa na Clinical officer aliyekuwa zamu. Ni binti wa miaka takribani 20 (kwa sababu za kimaadili sitataja jina, umri wake halisi, mahali anapoishi wala details zake nyingine). Hali yake ilikuwa mbaya maana alikuwa amenyong’onyea na alikuwa akipumua kwa shida sana. Mpira wa mkojo ulikuwa ukining’inia pembeni ya kitanda lakini hakukuwa na kitu ndani yake. Uso wake ulionekana kuvimba kwa mbali na alikuwa akizungumza kwa shida. Midomo ilikuwa mikavu na hata ngozi yake ilionekana iliyosinyaa na kavu kuliko kawaida. Nilimuita mwangalizi wake na kuanza kuchukua upya historia ya mgonjwa maana yeye mwenyewe alikuwa akizungumza kwa shida sana. Mwangalizi aliniambia kuwa mgonjwa wake, alianza kupata tatizo la kukosa mkojo kwa ghafla kama siku saba zilizopita. Hawakujua sababu hivyo wakadhani ni mambo ya ushirikina wakaamua kumpeleka kwa mganga wa kienyeji ambaye alikaa naye siku tatu huku akimnywesha kila aina ya miti shamba lakini bila mafanikio. Akasema, “tulipoona hali yake bado ipo vile vile tukaamua kumkimbiza hapa ili tujaribu huduma za kizungu. Kwahiyo kwa ujumla ana siku kama kumi tangu tatizo lilipojitokeza. Wakati tupo kwa mganga angalau hali yake ilikuwa siyo mbaya sana lakini jana usiku ndiyo hali ikabadilika tukaamua kumkimbiza huku. Sasa hivi hali chochote maana analalamika kichefuchefu muda wote, na akijaribu kula tu anatapika chote. Wakati mwingine anaongea vitu havieleweki basi baba ndiyo hivyo hivyo tu”. Baada ya kuuliza maswali zaidi kulingana na taratibu zetu, kwa muonekano wa mgonjwa na historia yake harakaharaka niliweza kuhisi ni kitu gani kitakuwa kinamsumbua huyu mgonjwa. Niliamua kumfanyia uchunguzi wa mwili (physical examination) ili kuona vishiria vingine vya ugonjwa. Alikuwa na dalili zote za mtu mwenye matatizo ya figo, na mbaya zaidi alikuwa katika hali ya hatari zaidi ya ugonjwa. Uchunguzi ulionesha, pamoja na dalili nyingine, kuwa alikuwa amevimba miguu (pedal edema) kwa kiasi fulani, tumbo lake lilishaanza kuvimba (ascites) na alikuwa akipumua kwa shida sana (dysponea), alikuwa na dalili za upungufu wa damu (anemia) na ngozi kavu kuliko kawaida kuonesha kuwa alikuwa amepungukiwa maji mwilini (dehydrated). Nikaagiza tufanye vipimo kadhaa kama vile vya kuchunguza utendaji kazi figo, vya kuchunguza uwiano wa madini/chumvi mwilini (electrolytes analysis), ultrasound ya tumbo, vipimo vya moyo na vipimo vingine kadiri nilivyoona inafaa. Ingawa vingi ya vipimo nilivyoagiza vilishindikana kufanyika ama kwa vile hakukuwa na vifaa vya kufanyia vipimo hivyo au hatukuwa na wataalamu wa maabara wenye ujuzi wa kufanya vipimo hivyo pamoja na kuwepo kwa mashine, bado niliweza kupata jawabu la tatizo lililokuwa linamsumbua mgonjwa wangu ingawa nakiri sikuweza kufahamu chanzo hasa cha ugonjwa wake ni nini kwa vile hatukuwa na vipimo vya kufanya hivyo. Alikuwa akisumbuliwa na kushindwa kufanya kazi ghafla kwa figo yaani Acute Renal Failure (ARF) na kwa dalili zake tayari alishafikia hatua ya kuwa na kiasi kikubwa cha madini ya potassium katika damu (hyperkalemia) na kwamba mrundikano wa uchafu mwilini ulikuwa katika kiwango cha hali ya juu kwa sababu figo zilishaacha kufanya kazi zake inavyotakiwa. Pamoja na kumuanzishia matibabu, katika hali aliyokuwa nayo matibabu sahihi ilikuwa kwanza kufahamu chanzo cha tatizo ili kukitibu, kumfanyia dialysis ili kutoa uchafu mwilini na hatimaye kama ikionekana figo zimekufa kabisa basi afanyiwe upandikizaji wa figo mpya. Nilipowaeleza yeye na mwangalizi wake kuhusu matokeo ya vipimo, hatua ya ugonjwa iliyofikiwa na nini cha kufanya ghafla niliona machozi yanamlengalenga mwangalizi. Kwa kweli alistahili kuwa vile. Kwa unyonge akaniuliza, “sasa baba hayo matibabu mnaweza kuyafanya hapa.” Nilimtazama tena na kwa kujitutumua ilibidi nimueleze tu ukweli kuwa hatuna uwezo wa kufanya dialysis pale kwetu, na wala hospitali ya karibu ya mkoa haina uwezo wa kufanya hivyo mjipigepige mumsafirishe mgonjwa Dar es Salaam kwa matibabu zaidi. Kama aliyekuwa anasubiri bomu zaidi nikamtajia na gharama za kufanya hayo matibabu na muda anaotakiwa kufanyiwa. Mama mwangalizi alinyamaza kwa sekunde kadhaa kama mtu anayefikiria kitu kisha kwa unyonge akasema , “baba kwa umaskini wetu huu hali yenyewe hii unaiona nilivyo. Naomba chonde chonde ujitahidi kufanya lolote lile hapa kama Mungu akipenda kumchukua basi mapenzi yake yafanyike maana hatuna uwezo wa kumsafirisha siyo tu kwenda huko Dar es Salaam bali hata hapo mkoani hatuwezi kufika”. Sikuwa na jinsi zaidi ya kuendelea na matibabu na kufanya kwa kadiri ya uwezo wangu kuokoa maisha ya mgonjwa wangu. Nasikitika kuwa baada ya masaa kadhaa mgonjwa yule alifariki kwa mshtuko wa moyo kama complication ya hypekalemia. Nilihuzunika sana lakini sikuwa na jinsi zaidi ya kuendelea kuchapa kazi kuhudumia wagonjwa wengine. Kwanini nimekikumbuka hiki kisa? Hiki ni kisa kimoja tu kati ya visa vingi vingi ambavyo madaktari wanakutana navyo kila siku katika utendaji wao wa kazi. Kushuhudia uhai ukipotea wakati ungeweza kuokoa maisha lakini huna vifaa au wataalamu wa kusaidiana nawe ni jambo linaloumiza sana kwa daktari na watoa huduma ya afya kwa ujumla wake. Nawafahamu madaktari waliowahi kufanya operesheni kwa kutumia mwanga wa tochi za simu baada ya umeme kukatika hospitalini kukiwa hakuna jenereta wala hata taa ya kandili, wapo waliolazimika kubuni mbinu mbadala baada ya kukosekana maji ya drip (iv fluids) kwa ajili ya matibabu. Hapa majuzi tumesikia kuhusu watumishi wa hospitali moja ya misheni huko mkoani Manyara wanaolazimika kutumia vipande vya nguo na mashuka kama gloves wakati wa kuhudumia wagonjwa, ipo mifano mingi mingi inayoonesha uzembe wa watendaji wanaotakiwa kuboresha mazingira ya kazi ili watoa huduma ya afya waweze kutoa huduma katika mazingira salama kwao wenyewe na kwa wagonjwa wao na hivyo kuokoa maisha yao. Kifo cha mgonjwa yule kingeweza kuzuilika au hata kucheleweshwa kwa mfano kama hospitali ya mkoa ingewezeshwa kutoa huduma ya dialysis kiasi cha kuweza kumkimbiza mgonjwa hospitalini hapo haraka. Lakini pia ingewezekana kuwa katika wakati mzuri wa kutambua chanzo cha ugonjwa wake kama hospitali ile ingekuwa na vifaa vya uhakika vya vipimo na pengine kulipatia ufumbuzi bila hata kuhitaji kumpa referral. Ipo mifano mingi yenye kufanana na hiyo. Mgogoro unaondelea hivi sasa nchini kati ya madaktari kwa upande mmoja na serikali kwa upande mwingine ni jambo linalosikitisha kutokana na jinsi suala hili lilivyoshughulikiwa na watendaji wakuu wa wizara pamoja na kuwa madai ya madaktari hawa ni ya msingi sana. Moja ya madai ya madaktari ni kutaka uboreshaji wa hospitali na vituo vyetu vya afya kwa maana ya vitendea kazi na mazingira ya kufanyia kazi. Dai hili siyo tu lina nia njema ya kuwahakikishia madaktari wanafanya kazi katika mazingira bora yenye vitendea kazi vya uhakika bali pia linahusu afya njema kwa ajili ya wananchi wenyewe. Kwa maneno mengine madai ya madaktari yanahusu pia ustawi wa afya za wananchi wengine na siyo maslahi yao tu binafsi. Ni aibu sana kwa hospitali ya Taifa, kwa mfano, kukatikiwa umeme bila kuwa na chanzo kingine mbadala cha umeme huku ukitegemea watoa huduma hawa kuacha kunung’unika. Haiingii akilini hospitali ya Wilaya kukosa hata strips za kupimia sukari mwilini na kisha ukategemea wafanyakazi wawe na furaha na kazi yao. Haingii akilini wauguzi wafurahie kufanya kazi kwenye wodi ambayo wagonjwa wamelala watatu watatu kwenye kitanda kimoja. Ni aibu, ni aibu, ni aibu. Pamoja na nia njema ya madai hayo, bado inasikitisha kuona jinsi ambavyo serikali kupitia kwa Waziri Mkuu walivyoona kuwa hakuna njia ya kuweza kushughulika na madai hayo zaidi ya KUAMURU madaktari kurudi kazini kana kwamba AMRI inaweza kuboresha mazingira ya kazi. Kumlazimisha tabibu pamoja na watoa huduma wengine wa afya kurudi katika mazingira yale yale wanayoyapigia kelele siyo tu hakutatui tatizo bali kunaongeza ukubwa wa tatizo. Hakuna tabibu na muuguzi atakayefanya kazi kwa moyo mmoja huku akiwa na hasira na kinyongo kwanza kwa kuamrishwa bila kusikilizwa anachodai lakini pili kwa kulazimishwa kurudi katika mazingira yaleyale anayodai yarekebishwe. Hatari ninayoina ni kwa wagonjwa kuzidi kupoteza maisha na wengine kuishia kupata vilema kutokana na matibabu butu watakayopewa na wahudumu wasioridhika. Na haya yakitokea wahudumu wa afya kamwe wasilaumiwe! Amri, vitisho, ubabe wala kamata kamata ya madaktari siyo suluhisho la matatizo. Ni matumaini yangu, wale wenye mamlaka wataona uzito wa madai ya madaktari na kuyapatia ufumbuzi wa kweli badala ya kuyapatia majibu ya kisiasa yenye vitisho na nia ya kufunika kombe ili mwanaharamu apite. Kinyume na hapo ni kuahirisha matatizo na kuendelea kuhatarisha afya za wananchi wengi masikini na wengine kufa kama yule binti. Lakini pia ni matumaini yetu, wananchi watatambua nia njema ya madaktari ya kutaka kuboreshewa mazingira yao ya kazi ili wananchi nao waweze kupatiwa huduma bora zaidi na uhakika tofauti na sasa. Ipo haja ya kuomba hoja ya dharura Bungeni ili kulizungumzia suala la mgogoro wa Madaktari na Serikali kwani hili ni suala linalouhusu umma wa Tanzania nzima. Wasipofanya hivyo itakuwa ni usaliti kwani raia wanakufa kwa kukosa huduma za wataalamu, wataalamu ambao wamedharauliwa kusikilizwa na kupewa majibu ya kuridhisha juu ya madai yao, kutoka kwa viongozi wa nchi wenye dhamana. Nimesikitika sana kusoma mahali ati, Waziri Mkuu na baadhi ya viongozi hawakutaka kuwafuata Madaktari kwenye kumbi walimokuwa wamekutania za Don Bosco wala Star Light hotel kwa kuhofia usalama wa maeneo hayo. Ikiwa Serikali ina waajiriwa wa intelijensia, usalama na polisi wanashindwa kuchunguza raia wao kiasi cha Viongzi kutishika, mwananchi wa kawaida anapaswa kuwa mashakari kiasi gani? Huu si udhaifu wa waziwazi? Hao walinda usalama kazi yao ni kuchunguza mitandao jamii na meseji za simu zinazohusu watu na mahawara zao tu? Ikiwa viongozi walihofia kwenda kwenye kumbi kuonana na madaktari, ni kwa nini madaktari wasihofie kwenda kuwaona viongozi hao? Kwa nini iwe sawa kwao na si sawa kwa wengine? Dhana ya uongozi kuwa kauli itatoka kwa kiongozi tu na mwananchi shuruti yake ni kupokea maelekezo daima dumu ni ya nchi gani? Sitaraji iwe Tanzania inayohubiri kuwa viongozi wake ni wasikivu kwa wananchi. Raia ndiye anayepaswa kutoa kauli kwa kuwa yote yanayofanyiwa kazi yanamhusu yeye, kawapa tu dhamana viongozi kusimamia. Hii nchi ya kuongozwa kwa kutisha watu haipo. Si sasa. Ile kasumba ya kutisha watu kama ilivyokuwa enzi za Mwalimu si wakati wake huu. Nayo imekwenda na aliyeileta, tusilazimishane. Huu ni upuuzi mkubwa kabisa kuwatisha watu kana kwamba ni wajinga na hawajui wanachokitaka. Hawa viongozi hawajajifunza yaliyotokea kwenye nchi nyingine? Uongozi wa mabavu huku mnajitapa mbele ya uso wa dunia kuwa ni nchi ya kidemokrasia ni upuuzi na ujinga wa hali ya juu. Kuwazuia watu kukutana katika kusanyiko la amani, ndani ya nyumba na si mtaani, ni kuua nguvu ya demokrasia ya uhuru wa kukusanyika na kuzungumza. Hawa Madaktari hawajaenda mtaani kuandamana, lakini kuwazuia kukutana ambako wamekuwa wakikufanya kwa amani hadi saa, ni dhahiri kuwa hatatakuwa na jinsi na hivyo wanalazimishwa kwenda mitaani. Nachelea kuamini kuwalazmisha kufanya hivi ni kwa lengo la kuonesha mabavu na ubabe. Ujinga ulioje! Kuwa Madaktari hawa baada ya kulazimishwa kutokukutana katika kumbi huru, basi watalazimika kwenda mtaani na huko ndiko nguvu ya mabavu itakapojidhihirisha kwa kuwapiga virungu, mabomu ya machozi na maji yanayowasha. Inasikitisha na kuhuzunisha kuwa ati hiyo ndiyo njia viongozi wanaojiita wenye upeo na demokrasia, wanaiona i sahihi, na ya kufuatwa. Madaktari si watu wajinga hadi wadai isiyo stahili kwa kazi zao. Ninaudhika sana kumwona daktari anataraji huruma ya mgonjwa ya kupewa chochote, “chakula cha daktari aka CCD” ili aifanye kazi yake bila kuwaza atakavyotimiza mahitaji ya nyumba yake. Ipo dhana nyingine, kwamba daktari wanapaswa kujiajiri. Hii ni dhana hafifu kwani maneno wanayosema watu wanaoshinikiza dhana hiyo hayaendani kabisa na 1. Kipato cha wananchi wanaopaswa ‘kukamuliwa’ malipo hayo. Ilivyo tu sasa wananchi hawawezi kujinunulia dawa au kulipia baadhi ya vipimo katika hospitali na zahanati za Serikali, wachilia mbali za binafsi. Watumiaji wakubwa wa huduma hizo ni matajiri na viongozi wa Kisiasa na Kiserikali, hao ni asilimia ngapi ya raia wote wa Tanzania? Raia wanaobaki watajipeleka wapi? Mtu unaposema waanzishe ‘private hospitals’ pia uangalie na jamii inayozungukwa. 2. Kipato cha daktari anayetakiwa kuanzisha hostpiali binafsi. Mshahara wa dakatri wa kati ya laki sita hadi nane, ni kiasi cha kuweza kutosha kudunduliza kuianzisha hospitali yenyewe? Ingekuwa ni cha kutosha, wangekuwa na haja gani ya kusumbuana na Serikali wakati huu? Unaposema wakakope, umenayafahamu masharti na ukiritimba uliopo katika kupata mikopo hiyo? Wapo waliofanikiwa kufanya hivyo, waulize ni kwa mbinu gani na "connections" gani walizozitumia. Isitoshe, mshahara gani huo utakuwa "guarantee" kumwezesha kupata mkopo Benki wa kutosha kujiunga na wengine kuanzisha hospitali binafsi? Matokeo yake si ndiyo kuwa na hostpiali zisizokidhi viwango? Kamati za Bunge si zimekutana nazo huko mitaani wakati wa ukaguzi na kuzifungia? Ninaudhika kweli ninapomwona daktari anahangaika kufanya kazi hospitali tatu (wenyewe huita viosk) ili aimudu familia. Si sahihi kumtwisha daktari, mwalimu, askari na kada nyingine mzigo wa kuombaomba na kutegemea huruma za wananchi ili kuendesha maisha. Si sahihi kumsababisha mwajiriwa yeyote aishi kwa kutegemea rushwa kutokana na mshahara usiokidhi mahitaji ya msingi. Ni dhambi na kufuru kumnyanyasa daktari, muuguzi, mwalimu n.k, kuwa kazi zao ni za wito kwa hivyo wanastahili kuwa na uvumilivu kana kwamba walijaaliwa roho ya ziada kuliko binadamu wengine, kwani ukweli ni kuwa walijaaliwa roho ya ziada ya kujali watu na si roho ya ziada ya kuonewa na kukubali uonevu. Hii dhana ya "kazi za wito" ndiyo inayohubiriwa na viongozi kwa nia ya kuwaziba midomo na kuwakandamiza. Kwani, kazi halali isiyo ya wito ni ipi? Si sahihi kulinganisha kada nyingine kusema mbona walimu, viongozi wa dini n.k. hawadai madai ya ziadana kuacha kumlinganisha na wafanyakazi wa sekta nyingine na viongozi wa Kiserikali/Siasa. Tukilinganisha kwa ‘kizio cha chini’ tukumbuke kulinganisha na kwa ‘kizio cha juu’ vile vile. Isitoshe, kwa kada na sekta nyingine kutokudai stahiki zao, hakumzuii daktari au muuguzi kudai yaliyo yake na yanayompasa. Kuwa mjinga na kuongozana kwenye kundi la wajinga ni kosa, ila mmoja katika kundi la wajinga anapoerevuka akajua anaonewa, anapodai haki yake, si mjinga huyo tena asilani. Na mjinga akierevuka, mwerevu yu mashakani. Madkatari msitetereke, vitisho havina budi kuja, hakuna popote ambapo imewahi kutokea 'smooth transition' hakuna, ni lazima kukubali kuingia hasara na gharama, pole ikiwa wewe ndiwe itakayekukuta, kumbuka hufanyi hivi kwa faida binafsi bali kwa ajili ya heshima yako ya sasa, kizazi kijacho na heshima ya “the noble profession”. Mwaka 2011, Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inasherehekea miaka ya uhuru wa serikali ya Tanganyika, taifa lililomezwa April 26, 1964 baada ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar. Kwa hesabu za haraka haraka utaona miaka hamsini ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itaadhimishwa April 26, 2014. Muungano wa Tanganyika na Zanzibar una faida na kasoro zake, lakini leo nitajadili mada inayouliza kuwa “baada ya miaka 50 ya uhuru wa Tanganyika, je Tanzania inakuhitaji?”. Magwiji na wataalamu wa falsafa ya imani duniani, wanatuaminisha kuwa hakuna nguvu inayozidi upendo, wakidadavua zaidi husema kuwa penye upendo uliopea Mungu yupo. Hata ukitafakari maisha ya mahusiano tunayoishi, huna budi kumpenda mtu kwanza kabla hujaenda mbele zaidi kumpa nafasi ya kuwa mwenzi wako wa ndoa, katika muktadha huo ni kawaida kumwona kijana mwanamke akitoka bara la Amerika kufunga ndoa na kijana mume toka Mwanza, vivyo hivyo haishangazi kuona vijana wakivuka bahari na mito, milima na mabonde kutoka bara moja kwenda bara jingine kutafuta mapenzi yanayojengwa na upendo. Hakika upendo ni nadharia ambayo hakuna maelezo yanayotosha kuidadavua kwa kilele chake. Bila shaka yoyote upendo miongoni mwa Watanganyika na Wazanzibar ndio uliozaa taifa la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa mtazamo wangu, upendo ule uliozaa muungano hapa Tanzania miaka 47 iliyopita, naona umepoa kama sio kufifia na kuchuja. Makala hii haitojadili nani amefifisha upendo huu hapa Tanzania. Nakumbuka siku ile, taifa lilipotangaziwa kuhusu afya ya baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere, kuwa hali yake sio nzuri, Watanzania tuendelee kumuombea, mwili ulinisisimka kwa hofu. Nikapata baridi na hofu kuu, maswali mengi yalinikaba hasa nikijiuliza, itakuwaje nchi yangu bila “a great man, father of the nation?”. Hakika Mwalimu Nyerere alikuwa “great man”. Hata viongozi waliomzunguka wao pia walikuwa “great people”. Watanganyika hawa “great people” kizazi chao shurti kiwe “great generation”. Wahenga walipata kusema kuwa “macho ni dirisha la fikra na ujasiri alionao mtu”, ukweli huu nauona kila ninapowatazama machoni Watanganyika nami nawaona kuwa na “great people”. Ujasiri huu tulionao hausemwi sana siku hizi, hivyo ipo haja ya kufanya kampeni ya makusudi miongoni mwa vijana wa Kitanganyika, hivyo upatapo fursa ya kushikana mkono na rafiki yako, vema ukamtazama machoni kwa walau dakika moja, kisha umwambie “you are a great person” kwa vile kila Mtanganyika ni kizazi cha “great people” ambacho ndio kiliasisi taifa la Tanganyika linalotimiza miaka 50 ya Uhuru tarehe 9 Desemba mwaka 2011. “Great people” wale wakiongozwa na “great man” Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere walifanikisha kujenga misingi ya Taifa la Tanganyika na kufanikisha Muungano wa Tanganyika na Zanzibar mwaka 1964, kwa vile upendo baina yao ulipea, vivyo hivyo waliipenda nchi yao na watu wake. Ukweli ni kuwa Watanganyika ni "great people", japo utamaduni wa kuambiana ukweli huu haupo tena nchini Mwetu. Nasisitiza kuwa Watanganyika ni kizazi cha “great people” kwa vile Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere aliweza kuwakaripia viongozi wa mataifa yenye nguvu za uchumi kama Amerika na Uingereza haya Israel pale alipoona matendo ya mataifa hayo yanaathiri kwa makusudi ustawi wa nchi zenye uchumi mdogo, kwa Mwalimu, kigezo cha ubinadamu hakikuwa uchumi bali ubinadamu wenyewe. Mwalimu Nyerere hakuishia kukemea mataifa makubwa pekee, bali alikemea pia viongozi wa ndani ya Tanganyika ambao nia zao binafsi zilikuwa zinakinzana na maendeleo ya nchi yetu. Mwalimu hakusita kuanika udhaifu, uchafu na tamaa za viongozi hao na akasisitiza kuwa watu hawa wasipewe uongozi kwa hawana nia thabiti ya kuweza ustawi wa jamii ya Mtanganyika. Bila shaka yoyote, msimamo huu wa Baba wa Taifa ndio ulikuwa msimamo wa serikali yake yote, ndio ulikuwa msimamo wa viongozi wengine wote, Mwalimu Nyerere amekuwa “father figure” kwa viongozi wengi wa Tanganyika kwa kuwa na maneno machache na matendo mengi, nakumbuka tulipata kuwa na wimbo wa kusifia matendo ya Baba wa Taifa kuwa “Raisi wetu hapendi kusema, raisi wetu Nyerere baba, anaonesha mfano kwa vitendo”. Mwalimu Nyerere alikuwa na shamba lake kule Butiama, shamba la Mwalimu lilikuwa mfano kwa wanakijiji wenzake, ukubwa wa shamba hili la Mwalimu haukuwa nusu ya ardhi ya kijiji, bali alichukua sehemu kidogo ili kila mwanakijiji mwenye nia ya kufanya kilimo naye apate ardhi. Hapa utaona fahari ya Mwalimu Nyerere haikuwa kujilimbikizia mali, ndio maana uwepo wa Tanzania ulimhitaji sana Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere. Swali linabakia, je baadhi ya viongozi tulionao ambao kujilimbikizia ardhi na mali kwa njia za ufisadi na kuuza mali asili zetu, Tanzania inawahitaji? Kwa vile utamaduni wa kuambiana kuwa “sisi ni great people”, imekuwa kawaida kuona Watanganyika wa leo tunaishi kama pimajoto -thermometer- ambayo inabadilisha kizio cha joto kadiri unavyoiweka kwenye nyuzi joto tofauti. Ni kawaida kwa pimajoto kusoma nyuzi joto za juu ukiiweka kwenye mazingira yenye joto la juu, pia ni kawaida sana ikiwa pimajoto itatolewa kwenye mazingira ya nyuzi joto la juu na kuwekwa kwenye barafu itasoma nyuzi joto sifuri ama chini ya sifuri. Mfano huu unamaanisha kuwa Pimajoto inaathiriwa na mazingira, hali inayotokea sana kwa Watanganyika wa leo bila kujali elimu zetu, vipato vyetu ama namna yoyote ya uelewa uliokolea, tumekuwa tunaathiriwa sana na mabadiliko ya agenda ama mazingira, kwa mfano bei za bidhaa zinapopandishwa kiholela tunalalamika lakini hatuchukui hatua kukemea na kukomesha hali hiyo, zaidi tumekuwa ni walalamikaji tuliojaa woga wa kuuliza kwa nini hali ipo hivi, nashangaa sana tumekuwa sio “great generation” tuliozaliwa na “great people” chini ya uongozi wa Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere ambaye agenda yake ilikuwa kukemea uoza huu. Mwalimu Nyerere na Waasisi wa Taifa letu hawakuishi kama Pimajoto, fikra zao hazikubadilishwa na mazingira kama ilivyo Pimajoto bali wao ndio walipambana kubadilisha mazingira magumu waliyokuwa nayo wakati huo hawakukubali chochote kilichodhalilisha utu wao, kilichobeza ubinadamu wao ama kilichodidimiza ustawi wa Tanganyika ama Watanganyika. Kwa kutunza heshima na utu wa Mtanganyika walisisitiza sana elimu ya ujamaa na kujitegemea. Ukitazama wengi wa viongozi tulionao Tanganyika ya leo wengi wanaishi maisha ya Pimajoto, wanabadilika badilika ili kufanikisha nia zao binafsi zinazokinzana na mahitaji ya mustakabali wa Taifa letu Tanganyika, baada ya miaka 50 ya uhuru wa Tanganyija, Watanganyika tunaoishi maisha ya Pimajoto, Tanzania inatuhitaji? Miaka 50 ya uhuru wa Tanganyika imeshuhudia awamu nne za maraisi wa Tanganyika, huku awamu ya kwanza ikiongozwa na Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere, awamu ya pili Mzee Ali Hassan Mwinyi, awamu ya tatu iliongozwa na Mzee Benjamini Mkapa na awamu hii ya nne usukani umeshika na Raisi Jakaya Kikwete. Katika awamu zote nne, serikali imepambana na changamoto mbali mbali za maendeleo, pia imetumia fursa nyingi za maendeleo ili kuwezesha maendeleo ya kiuchumi, kisisasa na ustawi wa jamii. Yatokanayo na jitihada hizi na changamoto zake sio muktadha wa makala hii. Kwa makala hii, miongoni mwa maswali ya kujiuliza ni:- je serikali ikiwa ni mzazi wa kila Mtanganyika, inawapokea Watanganyika na matatizo yao na kuwaongoza kutatua shida zao? Kwa maana jitihada zilizofanywa na awamu zote, miaka 50 baada ya uhuru wa Tanganyika zimefanikiwa kiasi gani kutatua matatizo yanayokabili ustawi wa jamii ya Mtanganyika? Je, miaka 50 inatosha tu inaalika sherehe na karamu ya kujivunia uhuru ama ni fursa kwetu kutafakari wapi tulipojikwaa kama Taifa badala ya kulalamikia wapi tulipoangukia? Maana miaka 50 ya uhuru wa Tanganyika haijatosha kutatua shida za msingi kama uhaba wa madawati mashuleni, uhaba wa madawa, vitendanishi tiba na watumishi hospitalini, kukosekana kwa nishati ya umeme ya uhakika na mambo mengine mengi. Kwa bahati mbaya sana miaka 50 baada ya uhuru wa Tanganyika , taifa letu linashuhudia matumishi ya ujuzi na utaalamu wa baadhi ya viongozi wenye tamaa, ulafi na ubinafsi vikitumika kuzidisha umaskini miongoni mwa jamii kubwa ya Watanzania, je, Tanzania itakapofikisha miaka 50, hapo tarehe 26 April 2014 itakuwa bado inahitaji viongozi wa namna hii? Nihitimishe kwa kusema kuwa, kila tunapotazama tulipotoka, hasa baada ya miaka 50 ya uhuru wa Tanganyika, vema tukijua kuwa sisi Watanganyika ni “great people” mambo yaliyofanywa na waasisi wa Taifa letu ni mfano hai wa hiki ninachosema. Changamoto tuliyonayo leo hii ni kuishi maisha ya Pimajoto, ambayo ni kinyume na silika ya “great people” maana “great people” wote huwa wanabadilisha mazingara yao na kuyafanya kuwa bora zaidi kwa ustawi wa taifa lao na vizazi vijavyo. Serikali haina budi kusimamia sheria zake ili wajanja wachache wasitumie maarifa waliyoyapata kuihujumu serikali, badala yake wataalamu hawa watumike kusaidia kusukuma mbele gurudumu la maendeleo ya Taifa, tukifuata njia hii ndiposa tutajibu hoja ya Miaka 50 baada ya uhuru wa Tanganyika, je Tanzania inanitaji? Imeandikwa na, Barnabas Mbogo. Nyamagana, Mwanza. Hivi ndivyo wanafunzi wanavyosoma usiku... 01/08/2011
...katika karne ya 21 wanayokuzwa wakiamini kuwa nchi tayari ina mkongo wa mawasiliano na hadi ifikapo 2010, eh, samahani, nadhani mwaka 20,100, shule zote za Tanzania zitakuwa zimeungwa katika mkongo wa mawasiliano... kwa sasa wavumilie tu kuvunzwa SIPIYU kwa nadharia. Akitoka hapo atakuwa na ujuzi wa kupambana vilivyo katika kutuma maombi ya kazi kwa njia ya barua pepe. Ataweza tu! Ajitahidi. Na, tusitarajie shule kuungua moto pia ati tu kwa vile wanatumia vibatari, koroboi na mishumaa. Vile vile madhara ya kupumua moshi wa koroboi kwa saa 2 - 4 mfululizo si mkubwa, tutafanya utafiti, wataalamu wetu wataona kama kuna madhara yoyote, watatushauri, tutajua la kufanya! Hivi moshi unafika ubongoni? sipati picha ambavyo ubongo ungekuwa unajaa weusi na ukungu wa moshi, hebu tusubiri wataalamu wetu watatufahamisha Sijui Bill Gates na Steve Jobs au Michael Dell ama Linux hawana mpango wa kutengeneza SIPIYU za mafuta ya taa? ah, nimesahau, mafuta ya taa yamepanda bei ni ghali pengine kuliko ya petroli/dizeli, ni vile watumiaji wa mafuta ya taa ni wachache kuliko wenye magari Tanzania lakini wenye maamuzi ya nchi ni wengi kuliko raia... I am sorry nime-mix huo mstari wa mwisho wengi ndiyo wachache na wachache ndiyo wengi... hebu pindua hapo utanielewa, nchi yenyewe tunasonga mbele kwa gia ya rivesi, n'shadata mie! Kwenda mbele kwa mwendo wa "reverse gear" nayo ni hatua jama! Kwanza tunajitahidi sana, ila ninyi hamuoni mazuri tunayofanya, mnalalamika tu! Hatuwezi kuwa na ufumbuzi wa matatizo yote, eenh, HAIWEZEKANI, kwanza matatizo yatakaa yaishe siku moja duniani? Likitoka hili, litakuja hili, na jingine na jingine, hayaishi! Ila sisi tunajitahidi kuyatatua kwa kadiri ya uwezo wetu. Huo ndiyo ukweli, hakuna ukweli mwingine zaidi ya huo. Wengine ni wabishi tuu, kwa kuwa wamezoea kubisha kila kitu. Eh, kwani sisi malaika bwana? Mnafikiri tungekuwa na uwezo wa kutatua matatizo yote tungeacha wananchi wateseke? Sisi tunasema hivi, eenh, kama kuna mtu anaona anao ufumbuzi wa haya matatizo, atuletee maelezo yake, sisi tutayafanyia kazi, sawa? eh eh e eh. Mgao wa umeme wamalizika nchini Tizamia 26/07/2011
Serikali ya Tizamia ambayo imekuwa kizani tangu kuzaliwa kwa nchi hiyo hatimae imefanikisha kumaliza tatizo hilo lililokuwa likiuvuta shati uchumi wake kwa miongo kadhaa sasa. Hayo yalisemwa jana na Mkuu wa Mamlaka ya Nishati wa Tizamia, Mh. Wiliamson Geresha, katika hotuba aliyoitoa katika moja ya vijiji ambako alikwenda kuzindua mradi mkubwa wa nishati mbadala (jua na upepo). Huku akishangiliwa na wanakijiji waliokuwa wakisikiliza taarifa yake kwa shauku kubwa, na pia akiwa amezingirwa na vyombo lukuki vya habari, Mh. Geresha alisema, "Kwa mara ya kwanza tangu dunia kuumbwa hatimae kijiji hiki cha Msonyo, na vijiji vingine 700 nchini kote, taa zinawaka na watoto wetu wanaweza kujisomea hadi usiku wa manane, baadhi ya wanakijiji wameweza kufungua saluni za kike na kiume, wapo waliofanikiwa kuanzisha biashara za kuuza vinywaji baridi na vikali na kutengeneza faida nzuri kutokana na kuwa na majokufu, baadhi ya vijana wameanzisha biashara za kuchaji simu, hongereni" Alisema Geresha huku akisikika kwa taabu kutokana na ushangiliaji wa muda wote wa wanakijiji. "Haya yote yamewezekana kwa usimamizi makini wa Serikali yenu ya Tizamia, ukusanyaji sahihi wa kodi ambazo badala ya kwenda kulipa posho za watawala, kununua magari ya kifahari, na kwenda kuwatibu watawala nje ya nchi na kufanya shopping baada ya matibabu, tumeweza kuwekeza kodi hizo katika manunuzi ya vifaa vya umeme-jua na upepo na kuvifunga bila malipo ya ziada katika nyumba ya kila mwanakijiji, zahanati, nyumba za ibada, bila kusahau sehemu za starehe kama bar na kumbi za muziki." Aliendelea kusema Mh. Geresha. Mbali na mambo mengine, Mh. Geresha pia alisema, "Serikali ya Tizamia kwa miaka nenda rudi imekuwa ikipiga maktaimu kukimbizana na vyanzo vya nishati ambavyo vimeshatutupa mkono, ila kwa kudra za Mwenyez Mungu, uongozi bora, na maono wa wananchi na watawala wa Tizamia, hatimae tumefunguka akili zetu na kuona ni kwa jinsi gani tulivyoacha jua linalowaka siku 365 za mwaka kupotea bure. Ni jambo lisilofichika kwamba kwa upatikanaji wa nishati hizi mbadala hakika tumefanikiwa kwa kiasi kikubwa kuongeza ukusanyaji wa kodi za serikali kwa sababu sasa wananchi wetu mmeweza kuanzisha miradi kadhaa inayowaingizia kipato, wananchi wanapata na serikali inapata, mambo waaaa!" Aliesema Mh. Geresha huku wanakijiji wa Msonyo wakimshangilia kufa na kupona. Upatikanaji wa nishati ya umeme ya uhakika katika nchi ya Tizamia ni hatua kubwa kuwahi kufanikishwa na serikali yake katika kipindi kisichopungua miongo minne. Matumizi ya nishati mmbadala ya umeme katika makazi ya watu kumetoa mwanya kwa umeme wa gridi ya taifa kutumika kwa matumizi makubwa kama ya viwandani na mashirika makubwa ya serikali. Viwanda vingi vikubwa vilivyokuwa vimefungwa vimeanza kufufuliwa tena na vingi vimekabidiwa kwa wawekezaji ambao ni wazawa wa nchi ya Tizamia. Pia pamekuwa na mfumuko wa kasi wa uzalishaji toka katika viwanda vidogovidogo ambavyo vingi viko maeneo ya vijijini. Viwanda hivi vidogo ni vile vya usindikaji matunda (ambayo awali yaliozea shambani), mbogamboga, vinywaji vitokanavyo na matunda n.k. Hii imewezesha Tizamia kuwa nchi ya wazalishaji na walaji, tofauti na hapo awali ambapo nchi hiyo ilikuwa ni soko na jalala la vyakula vya sumu pekee. Nilipopata wasaa wa kuzungumza na mwenyekiti wa kijiji cha Msonyo, baada ya Mh. Wiliamson Geresha kukamilisha hotuba yake, alinieleza haya, "Tangu kukamilika kwa mradi huu wa uwekaji wa umeme mbadala katika majumba yetu, kwa ruzuku ya serikali, tumeshuhudia wimbi kubwa la vijana wetu waliokimbilia mjini wakirejea na kutengeneza ajira hapahapa kijijini.""Ndungu mwandishi, jina la kijiji hiki ni Msonyo, jina hili lilitokana na hasira watu walizokuwa nazo kwa serikali yao ambayo ilikuwa ikiahidi tu kutuletea huduma hii na wasifanye hivyo. Msonyo ni jina lilitokana na usonyaji wa wanakijiji kila walipokuwa wakiona chochote kinachowakilisha serikali, iwe ni gari la mkuu wa wilaya, awe mwenyekiti wa kijiji, mjumbe wa nyumba kumi, au hata ofisi ya serikali za mtaa. Watu walikuwa wakisonya kuonesha dharau kwa ahadi za uongo za serikali ya Tizamia. Lakini sasa ni tofauti, tumepata nishati hii tuliyokuwa tukiisikia tu kwa wenzetu wa mjini, ambao nao hawakuifaidi sana pia kutokana na mgao. Kwa hili la kutupatia umeme ni jambo jema sana na hata uhasama kati ya raia na serikali yao sasa basi" alisema mwenyekiti huyo ambaye jina lake tumelipiga kabari. Naye Mh. Wilamson Geresha, Mkuu wa Mamlaka ya Nishati alikuwa na haya ya kusema, "Kwa kitambo sana serikali yetu ya Tizamia ilichukulia tatizo la ukosefu wa nishati ya umeme kama tatizo la msimu, tatizo linalotukumba wakati wa kiangazi na kusababisha ukosefu wa maji ya kusukumia mitambo ya kuzalisha nishati hiyo. Lakini baada ya miaka mingi serikali ikishirikiana na mchango wa kimawazo wa raia wake (ambao kwa miaka mingi tuliamini ni mbumbumbu), tuligundua kuwa tumekuwa tukipoteza sana kiuchumi na hivyo kuamua kulivalia njuga suala hiki kwa dhati kabisa." "Siyo serikali pekee iliyofanikisha hili, wananchi ndio hasa wahusika wakuu kutokana na kodi zao na mchango wa mawazo yao, halafu kuna wataalamu wa makampuni binafsi ya nishati hizi mbadala, ambao ndio waliofunga umeme huu nchi nzima, serikali mchango wake umeegemea zaidi katika kutengeneza sera za kumuinua mwananchi wake na kusimamia kwa dhati dhana ya uongozi bora na uadilifu wa viongozi." "Umeme huu wa jua na upepo ni ukombozi wa kweli kwa mwananchi wa Tizamia kwanu hawatatozwa tozo la mwezi zilizokuwa zinakusanywa na shirika la umeme la TANZU. Jua na upeo tunapata bure toka kwa Mungu kwa nini tuwatoze wananchi wetu? Sisi tutatoza kodi za haki zitakazotokana na uzalishaji wao. Tizamia Oyeee!" Alimaliza Mh. Geresha huku wanakijiji wa Msonyo wakimbeba juu juu kumpeleka kwenye gari lake. Nilishuhudia gari la Mkuu huyu lilisukumwa na wanakijiji hao hadi katika mpaka wa kijiji hicho. Ndugu msomaji, habari hii ni ya kufikirika, majina ya kijiji na mkuu wa nishati ni ya kufikirika. Ukishasoma habari hii POTEZEA. Tizamia Oye! (Itikia Oyeeee!). Swadaktaaa, tukutane wakati mwingine. HABARI KUTOKA: fotobaraza.me ...wakati kila kitu kimeondoka na kila kinga imemtoka mwanadamu, kinga ya mwisho inayosalia kabla hajavua nguo na kuingia mtaani akiwa mtupu, ni soni au haya. (Naomba kwa mara nyingine tusichanganye haya na aibu. Nimesikia na kuwasoma watu wakichanganya dhana hizi mbili. Napenda kurudia kwamba aibu ni fedheha inayotokana na tendo linalomvunjia mtu staha, kama kujikojolea hadharani au kumbaka mbuzi. Haya ni sifa ya kila mwana aliyelelewa vyema, mpole na mwenye heshima, staha na adabu). Sasa inaelekea tumebadhiri haya zetu kiasi kwamba tofauti yetu na kila kitoto kilichopitishwapitishwa maishani ‘fasta-fasta; bila kutoka jasho wala kutumia ubongo wake, ni kidogo sana. Hii inatokana na kuiga mambo ya hovyo kutoka kwa watu wa hovyo na utamaduni wao wa hovyo wakati tungeweza kuiga mambo ya maana kutoka kwa watu wa maana na utamaduni wao wa maana.... Tumbo liliovimbiwa linamdhuru binadamu kwa njia nyigi, mojawapo ikiwa ni kumpunguzia uwezo wa kufikiri. Ye yote aliyewahi kuvimbiwa (niliwahi kuvimbia nikiwa mtoto, kwa uroho) anaijua hali hiyo. Gesi zinazovurugana tumboni na kuzaa harufu chafu za mbweu, si tu zinakufanya usijisikie raha, ujihisi mchovu, lakini pia zinaondoa uwezo wa kufikiri.... Sijaelewa ni nini kinawafaya watu ambao wameapa kwamba dhamira yao ni kuwatumikia wananchi wazione ofisi zao kama mahali pa starehe. Kinachonishangaza zaidi ni kwamba inaelekea hakuna mkubwa ndani ya Serikali mwenye uwezo wa kuwaambia wenzake: Basi, inatosha, kifayyah! Rwanda alifanya Rais Kagame, lakini Kenya hawakumhitaji rais; alifanya Uhuru Kenyatta. Sisi hatunao watu kama hawa? Soma makala nzima yenye kuunganisha vionjo hivyo kupitia raiamwema.co.tz (bofya hapa) Hoja ya kumjibu Rostam Aziz 15/07/2011
Naam! kwa hili siwezi kukaa kimya, siwezi kukubali linipite kirahisi rahisi hivi ndivyo navyoanza uchambuzi wangu huu wa leo ambao unalenga kujadili kwa undani kuhusu hotuba ya Rostam Aziz aliyoitoa juzi tarehe 13 siku ya jumatano mwezi huu mwaka 2011 huko Igunga wakati akitangaza rasmi kujiuzulu Ubunge na ujumbe wa kamati kuu ndani ya CCM. Nitamulika kipengele kimoja baada ya kingine kwanza kwa lengo la kuwaelewesha wasomaji wangu mtazamo wangu lakini pili ni kumtumia ujumbe Rostam na wafuasi wake kuwa watanzania tupo macho tunafatilia siasa za nchi yetu mwisho wa yote kwa vile hotuba ya Rostam ilikuwa imejengwa kwa misingi ya hoja, mantiki na ufundi mkubwa wa fasihi nami nitatembea kwa mapigo hayohayo ya hoja, mantiki na fasihi. Naam! kwa hili siwezi kukaa kimya, siwezi kukubali linipite kirahisi rahisi hivi ndivyo navyoanza uchambuzi wangu huu wa leo ambao unalenga kujadili kwa undani kuhusu hotuba ya Rostam Aziz aliyoitoa juzi tarehe 13 siku ya jumatano mwezi huu mwaka 2011 huko Igunga wakati akitangaza rasmi kujiuzulu Ubunge na ujumbe wa kamati kuu ndani ya CCM. Nitamulika kipengele kimoja baada ya kingine kwanza kwa lengo la kuwaelewesha wasomaji wangu mtazamo wangu lakini pili ni kumtumia ujumbe Rostam na wafuasi wake kuwa watanzania tupo macho tunafatilia siasa za nchi yetu mwisho wa yote kwa vile hotuba ya Rostam ilikuwa imejengwa kwa misingi ya hoja, mantiki na ufundi mkubwa wa fasihi nami nitatembea kwa mapigo hayohayo ya hoja, mantiki na fasihi. UTANGULIZI Katika sehemu hii ya hotuba ya Rostam anasema kuwa ameamua kuzungumza na “wazee wa Igunga” , hapa kuna jambo linajificha, tena kuna utata mkubwa sana wa Rostam kuamua kuzungumza na wazee, kuzungumza na wazee ni style aliyokuwa anaitumia Mwalimu Nyerere wakati akizungumza mambo mazito na wazee wa Dar es salaam, kwa maana nyingine mantiki ya Rostam kuzungumza na wazee wa Igunga inalenga kutuhabarisha kuwa alikuwa akizungumza mambo mazito? Sasa je kujiuzulu kwake ni jambo zito kwa nani? kwa wana Igunga? Wazee wa Igunga? WanaCCM? Au watanzania? Kwanini liwe jambo gumu? Mbona hata Nyerere na Kawawa waliwahi kutoka kustaafu uongozi CCM? je Rostam ni nani ndani ya CCM? je upi uzito wa Rostam? YATOKANAYO Hapa Rostam anaonyesha wazi yeye ni mtu wa namna gani? tena anasisitiza kwa maneno haya “Nyinyi wenyewe ni mashahidi wazuri kwamba tangu matukio yanayogusa jina langu yaanze kutokea miezi michache tu baada ya serikali ya Awamu ya nne inayoongozwa na Rais Jakaya Kikwete kuingia madarakani mwaka 2005, tumekuwa tukiyapuuza na kuendelea kufanya kazi kwa bidii”, sasa hapa Rostam anasema alikuwa anayapuuza matukio yale, hebu tujiulize kwanini mtu anapuuza kitu? Mtu makini ni yupi anayepuuza au anayechukua tahadhari? Je tukisema dharau na kupuuza kwake leo hii kumemlazimisha kutema ubunge na ujumbe wa NEC tutakuwa tumemwonea? Labda niseme wazi kuwa Rostam siyo kwamba alikuwa anapuuza bali kinachoonekana minyukano ya kimakundi ilipamba moto na kujikuta wenzake wamemzidi kete kiasi kwamba hata utetezi wake ungepuuzwa, kwani mara ngapi alijaribu kujitetea? Au tupige kura tubaini watanzania wangapi wanamwona Rostam msafi? Kupuuza haimaanishi ni msafi ila wakati mwingine yaweza kuwa ni tuhuma za ukweli kiasi kwamba mtu anashindwa hata kujitetea. KUJIVUA GAMBA Hapa Rostam anaonyesha jinsi gani anavyokwepa ukweli, anaacha kusema waziwazi kwa mhusika anawageukia Nape na Chiligati, hivi Rostam anataka tuamini kuwa wanachokifanya Nape na Chiligati hakina baraka za Kikwete? Hivi ndo tuseme Nape na Chiligati ni waropokaji majukwaani? Hawajatumwa na Kikwete? Tukiamini hivi tutakuwa kama tunakimbia ukweli ambao ni lazima tutakutana nao mbele tu, kwa kifupi Rostam alikuwa anamsuta swahiba wake Kikwete kwa mgongo wa Nape na Chiligati. Kwanza kabisa Rostam anamaanisha kuwa Kikwete anang’ata na kupuliza kwa maana yeye hakusema kwenye kamati kuwa “magamba” lazima waondoke ndani ya siku 90 lakini wakati huohuo Rostam hajasema iwapo Kikwete aliwahi kuwaonya Nape na Chiligati kuwa waache kujitungia maneno yao hivyo Rostam anamaanisha kuwa Kikwete alikuwa nyuma ya Nape na Chiligati hivyo Rostam anaonesha jinsi gani swahiba wake Kikwete amemwacha asombwe peke yake na mawimbi ya minyukano na makundi ndani ya chama. MAAMUZI YANGU Hapa ndipo ambapo Rostam kaniacha mdomo wazi na imani sio mimi peke yangu bali wengi wameshangaa kauli zake zilizojaa ubinafsi. Rostam anasema kuwa hana ameamua kuacha uongozi kwasababu siasa za kupakana matope zinamjeruhi kibiashara, hivyo Rostam kaona bora biashara zake kuliko wananchi wa Igunga halafu “eti nimesikia wanamlilia” ajabu sana , hapa kuna mambo mawili matatu yaliyojificha, la kwanza ni kuwa Rostam kwake biashara kwanza na kuwatumikia wananchi ni kiporo tu, pili tunarudi kulekule wafanyabiashara wengi wanawania ubunge ili kulinda maslahi yao ya kibiashara na si vinginevyo na tatu laana ya baba wa taifa inatuandama aliwahi kutuonya kuwa makini na matajiri wanaojichomeka kwenye siasa tuwahoji mara mbilimbili nia yao , sasa nadhani watanzania wameona kuwa wafanyabiashara huwa wapo kimaslahi na wanapoona hawapati basi hawaoni kazi kuchukua uamuzi wowote hata ikibidi kujiuzulu. HITIMISHO Naomba nihitimishe kwa kutoa mapendekezo kadhaa; Kwanza kabisa mpaka sasa Rostam hajaonyesha kupinga shinikizo la Nape la kumtaka kung’atuka, hivyo amekubali kosa , siwezi kujadili maneno yake kuwa hakubaliani na shinikizo kwasababu ikiwa anapinga shinikizo la Nape na Chiligati basi hakupaswa kujiuzulu badala yake alipaswa kwenda mahakamani kupinga kudhalilishwa au angewataka wanaomtuhumu kumfikisha mahakamani. Pili Rostam aache kuwafanya watanzania watoto eti kwa kauli kuwa ataendelea kuwa mwanachama mwaminifu wa CCM, nani kasema? Nasema labda Nape na Chiligati waondoke vinginevyo ni swala la muda tu ila misuguano itaendelea tu. Tatu natoa wito kwa Kikwete ajivalishe nafasi ya Nyerere, je angekuwa Nyerere angefanya nini? je angevumilia mazingaombwe “CHAPA KUJIUZULU” au angeongeza na “CHAPA TAIFISHA MALI ZAO” , Naam nasema tena “vision 2015” itazidi kuiyumbisha CCM , naona wapigane na mfumo mbovu ambao usiwe na mipaka hata ikibidi serikali kung’oka naona ing’oke tu ili kunusuru nchi vinginevyo kwa mbali naanza kuamini utabiri wa baba wa taifa aliposema “CCM watakapoanza kugawanyika mjue itaanguka” na huu kama si mgawanyiko ni nini basi? Tafakari! Nova Kambota Mwanaharakati, +255717 709618 novakambota@gmail.com www.novakambota.com Tanzania, East Africa Ijumaa, 15 julai, 2011. Siri ya mafanikio: Ufugaji - Mifano ya wanaovuna zaidi ya milioni 7 kwa mwezi mbali na mshahara! 10/07/2011
Tumekuwa wazuri sana kwa kupiga kelele kwamba Serikali hivi, Serikali vile, Viongozi hivi, Viongozi vile, tukiendelea kuamini maneno yao ya 'kutuletea maisha bora' wakati ukweli ulio dhahiri ni kuwa, kamwe Serikali haitatuletea chakula mezani bali kwa juhudi za mikono yetu wenyewe. Mifano hai ya juhudi zenye malengo ni kama mtaalamu Kanja wa masuala ya IT (Information Technology) ambaye alikuwa na ndoto za kununua gari zuri aina ya Audi, lakini punde fedha ya kununulia gari ilipopatikana, akabadili mawazo na kuamua kufanya ufugaji "ranch" na sasa anajiingizia faida ya shilingi za Kenya zaidi ya 400,000 (sawa na zaidi ya shilingi 7,000,000 za Kitanzania; shilingi 1 ya Kenya = shilingi 18 za Tanzania) kwa shughuli ya ufungaji tu, mbali na mshahara wa ajira yake ya utaalamu wa IT. Mwendelezo wa mahojiano ya Jeff Koinange na Douglas Kanja yanapatikana youtube (bofya hapa). Jeff pia amewahoji wafugaji wengine ni Njeri Gota (bofya hapa) na John Gethi (bofya hapa). Hakuna kazi yenye faida rahisi, lakini ukweli pia ni kuwa, kila mafanikio yanahitaji nia na juhudi. Hivi Watanzania tutaendelea kuwalalamikia Wakenya hadi lini kwa madhaifu ya kurekebisha wenyewe? 08/07/2011
"nakupenda", "unakaa wapi?", "unasoma au unafanya kazi?", "naweza kukuona?", "naomba namba yako ya simu", "wewe mzuri... Nimeshangazwa, si mara moja, mbili au tatu, ni zaidi. Kinachonishangaza na kunitia simanzi ni jinsi ninavyowasoma watu kwenye blogu, e-groups, e-forums na tovuti, ambazo yapo matangazo ya nafasi za masomo au kazi zinazowahusu Watanzania, lakini mara nyingi nafasi hizo zinachangamkiwa zaidi na jirani zetu Wakenya. Mathalani ni kazi ya kutafsiri ambayo nimeinukuu na kuimeibandika hapo chini. Ukiitizama, wengi waliojitutumua ni Wanaigeria au Wakenya. Pengine tutajitetea kuwa Naigeria ina wakazi wengi na raia wengi waliotawanyika kote ulimwenguni, je, kwa Kenya tutajiteteaje? Idadi yao ya raia kweli ni tishio kwa Tanzania hata waweze wao kuchangamkia fursa hizo zaidi yetu sisi? Hata ikiwa matumizi ya TEHAMA kwa Wakenya ni kubwa zaidi ya ile ya Watanzania kwa sababu kadha wa kadha ikiwamo matatizo ya umeme na jamii kubwa kutokutumia tarakilishi; Ninakataa dhana hiyo kwani ipo idadi ya Watanzania wengi ambao huperuzi blogu na tovuti mbalimbali za habari na pia wapo sana kwenye mitandao jamii kama faceboook na twitter. Cha ajabu, nikitizama walio wengi katika kundi langu la marafiki (ninao wafahamu na nisiowafahamu) mengi ya wanayozungumzia ni mambo yasiyo kuwa na kichwa wala mkia, aghalabu, mambo yasiyoweza kumsaidia katika kujijazia elimu na maarifa bora. Wanaotoa maoni mengi huegemea zaidi upande wa siasa, tena siasa za lawama na siyo siasa za nini cha kufanya ili kusaidia kuondokana na hali duni. Inakuwa kama vile kila siku mtu anataka kurusha lawama kwa watu au kundi fulani, kisha anajisikia vizuri kuwa naye siku hiyo ametoa machungu yaliyo moyoni. Sasa kusema tu bila kutenda kwa mfano kuna faida gani? Kama ni kuzungumza na kusema mbona yayo hayo yanasemwa na kurejelewa siku nenda rudi, kwani wanaopaswa kusikia hawajasikia? Hilo halitoshi kuwa funzo kuwa mbinu ya kupiga domo mfululizo tu si hoja tena? Kila mtu tu aseme, nani asikilize? Sisi tukiendelea kupiga kelele, wenzetu Wakenya, pamoja na kupiga domo huku na huko kwa mambo yasiyo na kichwa wala mkia, bado wanaongoza kwa kuchangamka kutafuta ziliko nafasi za kazi mitandaoni. Hivi sisi tutabaki tunawapigia kelele Wakenya kwa kufanya hivi na vile hadi lini badala ya kuchangamka? Kwa kweli ninakereka ninapoona wengine wanajitahidi kusambaza nafasi za elimu na kazi, lakini bado ni kama vile walengwa wamevuta shuka na kugeukia upande wa pili. Tutasaidiana vipi ndugu, jamaa na marfiki zetu ikiwa wengine wanabakia tegemezi na kuomba omba tu? Watanzania wenzangu, tuwahimize watumiaji intaneti wanapofika kwenye intaneti kuwa jambo la maana na muhimu kufanya ni kuperuzi tovuti zenye nafasi za kazi, shule na zile zenye taarifa chanya zinazoihusu jamii. Watu wasiishie kuweka "status update" kwenye facebook na twitter na kutumiana tu jumbe za "nakupenda", "unakaa wapi?", "unasoma au unafanya kazi?", "naweza kukuona?", "naomba namba yako ya simu", "wewe mzuri..." maoni (comments) yasiyo na tija! Habari ya kazi ya kutafsiri niliyoitolea mfano ni hii ifuatayo [inapatikana: freelancer.com]:- Hi All, I have a translation project from english to Swahili, Igbo, and Afikaans. I want to be ready with some freelancers or companies to help me with these translation. Please send me your fees per 1000 words. Also, let me know your daily output. Budget: $250-$750 USD Created: 06/26/2011 at 18:16 EDT Bid Count: 13 Average Bid: $373 USD Ends: 07/01/2011 at 18:16 EDT | Vitabu vya WatanzaniaBofya picha ya kitabu unachokitaka ili ujinunulie nakala
Yaliyomo/CategoriesAll Hifadhi/ArchivesFebruary 2012 |














RSS Feed