wavuti
wavuti logo Facebook icon Facebook icon Twitter icon Subscribe RSS
 
Picture
Mwenyekiti wa CCM Taifa Rais Jakaya Kikwete alifungua harambee ya kuchangia fedha uchaguzi mkuu CCM mkoa wa Kilimanjaro iliyofanyika katika hoteli ya Golden Tulip jijini Dar es Salaam. Harambee  hiyo ilichangisha jumla ya shilingi za Kitanzania Milioni Mia Mbili (200, 000, 000/-).

YATOKANAYO
Ni mengi. Nimeshindwa niandike lipi na lipi niache. Tafakari wewe!
 
 
Picture
Dakika kadhaa zilizopita nilikuwa nikitazama ukurasa wangu wa facebook. Nilishtuka sana baada ya kusoma maoni ya mmojawapo wa marafiki zangu. Sikuamini alichoandika ilibidi nikirudie mara mbili mbili kujiaminisha ndicho. Kifupi alikuwa anamueleza rafiki yetu mwingine kuwa yeye hajajiandikisha kupiga kura na wala hana mpango wa kwenda kupiga kura wakati wa uchaguzi mkuu wa mwaka huu.

Nilishtuka sana kwa sababu kuu mbili. Kwanza sikutegemea uamuzi kama ule utoke kwa kijana msomi kama yeye. Lakini pia sikutarajia uamuzi kama ule utolewe na kijana anayelilia mabadiliko katika nchi yake.

Nilishindwa kujizuia, nikaamua kumuuliza kujiaminisha kuwa asemacho ndicho, na ndivyo alivyokiri kwa hakika kabisa kuwa hatapiga kura. Sababu kuu zikiwa haoni ni kwanini apoteze muda wake kupiga kura wakati anadhani hakutakuwa na mabadiliko yeyote na hivi kupiga au kutokupiga kwake kura hakutaleta tofauti yeyote. Lakini jingine lililomfanya afikie uamuzi huu ni kuwa hotuba ya mheshimiwa Rais ambayo kwake anasema ilimkatisha tamaa na hakuona umuhimu wa kupiga kura tena.

Uamuzi wake huu bila shaka unaakisi kelele za muda mrefu kuhusu ushiriki wa vijana katika uchaguzi wa viongozi wa Taifa letu. Ni mara kadhaa tumesikia watu ama makundi ya watu wakisisitiza kuhusu umuhimu wa vijana kushiriki katika kupiga kura ama hata kugombea uongozi.

Wakati wa uchaguzi mkuu wa kwanza wa vyama vingi wa mwaka 1995, mgombea mmoja wa urais kwa chama cha upinzani alidanganywa na idadi kubwa ya vijana waliokuwa wakijitokeza kwenye mikutano yake ya kampeni. Kundi hilohilo pia lilikuwa likijitokeza katika kulisukuma gari lake na kumshangilia, lakini ambacho mgombea yule hakuelewa ni kuwa vijana wale wala hawakuwa wamejiandikisha kupiga kura wala hawakupiga kura. Na hivi hata idadi ya kura zake haikuwa kama alivyotarajia. Hapo utaona kuwa kumbe vijana wale walitamani mabadiliko lakini walitaka mabadiliko hayo yaletwe na nani na kwa njia gani kama si wao kujiandikisha na kupiga kura?

Swali la kujiuliza hivi ni kwanini vijana hawapendi ama hawataki kujihusisha katika kuchagua au kuchaguliwa? Inawezekana kukawa na majibu mengi kwa kila mmoja wetu, lakini je hayo majibu yanatosheleza sababu za kutokutumia haki yako ya kikatiba ya kuchagua au kuchaguliwa?

Ifahamike kwamba katika kufanya mabadiliko kuna kadhaa lakini zilizo kuu ni mbili, ama za kutumia demokrasia au kutumia mabavu katika kuuondosha au kuubadilisha uongozi uliopo. Na katika nchi inayojidai inajiendesha kidemokrasia hili la kwanza ndilo linalotumika. Sasa inapotokea kuwa kundi kubwa zaidi katika jamii ambalo ndilo kwa namna moja ama nyingine litaathirika na maamuzi yatakayofanywa na kundi dogo halitaki kutumia fursa yake katika kufanya maamuzi, hali hiyo si ya kufurahisha hata kidogo.

Vijana wa Tanzania ambao ndo wazalishaji na wajenga nchi wakuu, wana kila sababu ya kuhitaji mabadiliko. Wana kila sababu ya kuhitaji maendeleo yanayoendana na umri wa nchi yetu, wana kila sababu ya kuhitaji hali bora kwa ajili yao na wazee wao pamoja na wadogo na watoto wao. Lakini kwa vile mabadiliko hayaji kwa kusubiri mwingine akae kukufanyia maamuzi, ni jukumu letu vijana kuhakikisha tunashiriki katika kuleta mabadiliko haya, ama kwa kupigiwa au kwa kupiga kura.

Vijana tunapolalamika kuwa kiongozi fulani hafai kwa sababu hafanyi hivi au hivi au tunataka hiki na hiki na yeye hakitimizi wakati hatukupiga kura kumkataa tutakuwa hatujitendei haki sisi wenyewe na wala hatuwatendei haki wenzetu. Kupewa nafasi uifanyie kazi halafu huifanyii, lolote baya likitokea basi nawe pia unahusika katika kutokea kwake na hivi huna haki ya kulalamika.

Kwa hivi vijana, sisi ambao tunafanya kundi kubwa la jamii ya watanzania tutumie nafasi yetu tuliyonayo katika kupiga kura kuwakataa wagombea wote ambao tutaona hawafai  na wale ambao wana uwezo wa uongozi tuchukue nafasi hii kugombea nafasi mbalimbali za uongozi kwa manufaa ya Taifa letu.

Taifa linahitaji mawazo mapya, taifa linahitaji sura mpya, taifa linahitaji nguvu mpya. Lakini hivyo vyote vitatoka wapi kama sisi vijana tutakaa kuachia wengine watupigie kura na kutuchagulia watu walewale, wenye sura zilezile, wenye muono uleule, wenye mawazo yaleyale ya kichovu yasioendana na mabadiliko ya ulimwengu kwa sasa.

Kijana fahamu kuwa usipopiga kura umeisaliti nafsi yako, umetusaliti vijana wenzako wenye kutaka mabadiliko ya maendeleo ya kwenda mbele (maana kuna mabadiliko ya mendeleo ya kurudi nyuma pia), umewasaliti wadogo zako wanaokutegemea na umewasaliti watoto wako ambao kesho watakuuliza mama au baba ulikuwa na nafasi ya kuleta mabadiliko kwa kupiga au kupigiwa kura lakini hukutimiza wajibu wako. Na hapo sijui utajitetea nini.

Tanzania yenye mabadiliko inawezekana, acha kulalamika na kulalamikia viongozi wasiofaa, timiza wajibu wako, waondoe madarakani.

Mungu Ibariki Tanzania, Mungu tubariki vijana. 

Monsignor
"Mtaka cha uvunguni, inua kitanda juu"

 
 
Mkazi mmoja wa Kijiji cha Kijerwa Hemsambia kata ya Kigongoi wilayani Mkinga mkoani Tanga amewateka nyara watu wanne wa familia moja na kumnyonga mtoto mdogo mwenye umri wa miaka minne ambaye ni mpwa wake.

Mtekaji nyara huyo, Mwajego Jumaa, anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka 20, aliifungia familia hiyo ndani ya kibanda porini kwa muda wa siku tatu mfululizo kisha kumuua mtoto mmoja ambaye jina lake halikuweza kupatikana mara moja.

Baada ya kutekeleza mauaji hayo, kijana huyo aliichukua maiti ya mtoto huyo na kuiingiza kwenye mfuko wa kiroba na kisha kuitupa porini.

Kijana huyo anasadikiwa kutumia silaha mbalimbali likiwamo panga, upinde, manati na mbwa wanane katika kufanikisha kazi hiyo ya utekaji nyara huo, akiwamo dada yake, kaka na wapwa zake wawili.

Kufuatia tukio hilo, wananchi wa Kijiji hicho walitoa taarifa katika kituo Kikuu cha Polisi Maramba ambapo Askari wa Kutuliza Ghasia (FFU) walikwenda kijijini hapo na kisha kufanikiwa kumtia mbaroni.

Mmoja wa wananchi wa Kijiji hicho ambaye hakutaka kutaja jina lake gazetini alidai kuwa mtuhumiwa huyo anadaiwa kuwa tatizo la ugonjwa wa akili na inadaiwa alikuwa akijihusisha na kilimo cha zao la bangi katika shamba lake.

Akizungumza na gazeti hili, Mkuu wa Upelelezi Mkoa wa Tanga, Jaffar Mohamed, amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kueleza kuwa kwa sasa mtuhumiwa anaendelea kushikiliwa na Polisi huku uchunguzi zaidi wa tukio hilo ukiendelea. Mara baada ya uchunguzi huo kukamilika, mtuhumiwa huyo atafikishwa mahamani kujibu tuhuma zinazomkabili.

Credit: DarLeo
 
 
Katibu wa CCM kata ya Isamilo jijini Mwanza Bw. Bahati Stephano (49) ameuawa kwa kuchomwa kisu mara baada ya kuvamiwa ofisini kwake na kijana mmoja aliyetambulika kwa jina la Jumanne Oscar (30).

Tukio hilo limetokea leo majira ya saa sita na nusu mchana mara baada ya kijana Jumanne Oscar kuvamia ofisi hizo na kumkuta katibu huyo na kisha kuzuka majibizano ya maneno ambayo yalisababisha kijana huyo kuchomoa kisu na kumchoma Katibu huyo upande wa kushoto wa kifua na kisha tumboni.

Katibu huyo wa CCM kata ya Isamilo alifariki njiani wakati wakiwa anapelekwa katika Hospitali ya rufaa ya Bugando kwa huduma.

Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo, kamanda wa polisi mkoa wa Mwanza Bw. Simon Siro amesema mara baada ya kufanya ukatili huo kijana Jumanne Oscar alitoka ofisini humo akikimbia kuelekea Ziwani lakini kwa nguvu za Wananchi alikamatwa na kupelekwa katik kituo cha polisi kwa mahojiano zaidi.

Credit: Albert G. Sengo, Mwanza
 
 
Wananchi wa Mbezi Mtoni, kata ya Kawe wameandamana kupinga uongozi wa Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa huo, ambaye ameingia madarakani hivi karibuni kwa kuchaguliwa na wananchi, kutokana na Mwenyekiti huyo kudaiwa kuuza maeneo ya wananchi yaliyotengwa kwa ajili ya maendeleo bila kuwashirikisha.
Picture
Wakazi hao wa Mbezi mtoni walionekana na bango lililokuwa likisomeka ‘Sasa umeingia Tarime Full Machafuko’, huku wakiwa na mapanga wakilinda maeneo ambayo bado hayajauzwa baada ya kuona watu wasiojulikana wakirandaranda katika maeneo hayo na mwenyekiti huyo.

Vijana wa maeneo hayo waliamua kujikatia maeneo yaliyokuwa yamebakia na kuweka alama za kumiliki maeneo hayo baada ya kuona Mwenyekiti huyo amezidi kujichukulia maamuzi na bila kutoa taarifa kwa wananchi kuhusiana na ujenzi aliokwisha uanza anaodai ni Hospitali ya yenye thamani ya shiilingi milioni 20.
 
Wananchi hao walikutwa wamekusanyika katika msingi ulioanza kujengwa ambao umeelezwa kuwa ndiyo hasa hospitali ambayo wananchi wanaipinga kutokana na gharama zilizotajwa na hali halisi inayoonekana.

Picture
Waandishi wa habari walifanya jitihada za kumtafuta Mwenyekiti huyo na kufanikiwa kumkuta katika ofisi ya Serikali ya Mtaa, ambayo tayari nayo ilikuwa imezingirwa na wananchi wenye hasira huku wakiimba kumshinikiza kujiuzulu madaraka kutokana na uongozi wa ubabaishaji.

Baada ya Mwenyekiti huyo aliyejitambulisha kwa jina la Joseph Benjamin kuulizwa kuhusiana na ujenzi wa hospitali hiyo una baraka zozote za wananchi ama Kamati ya Maendeleo ya mtaa huo, alijibu kuwa alishafanya vikao vingi kuhusiana na ujenzi huo na kuhusiana na kuwaongoza wananchi hao kibabe alidai kuwa, anaamini hao waliofikisha malalamiko hayo ni wale tu ambao amekuwa akikataa kuwanunulia bia pindi wanapokutana katika Baa.

Picture
Alipotakiwa kuonyesha karatasi za kumbukumbu za vikao vilivyopita vinavyohusu ujenzi wa hospitali hiyo, aliwataka waandishi wa habari kumpa muda na kuahidi warudi siku ya pili yake ili kuandaa na baada ya kubanwa na kupewa muda wa saa moja alisimama na kuelekea nyumbani kwake iliyo umbali wa mita 15 hivi kutoka ofisi hiyo, huku akizomewa na wananchi na baada ya dakika 38 alirejea akiwa na karatasi hizo. Baada ya kufika alipoanza kuonyesha kwa waandishi wa habari zilionekana ni za vikao vilivyopita vya maendeleo ambavyo havikuwahi kufikia muafaka wala makubaliano kama ilivyoelezwa na wananchi hao. Naye Mwenyekiti wa Kamati ya Maendeleo ya Mtaa huo aliyejitambulisha kwa jina la Fredick Ngonyani, alipoulizwa kuhusiana na ujenzi huo alidai kuwa hauna baraka zozote za Kamati hiyo wala wananchi badala ya kuona tu mafundi wakianza kujenga.

“Hatujui pesa zinazotumika katika ujenzi huo zimetoka wapi wala wakandarasi wa ujenzi huo hatuwatambui, wala mwekahazina ila tunaona tu ujenzi ukiendelea, na tunapohoji kuhusiana na ujenzi huo tunajibiwa hatuna madaraka ya kuhoji kwani yeye ndiyo Mwenyekiti aliyechaguliwa na watu wengi” alisema Ngonyani.

credit: Muhidin Sufiani & ITV

 
 
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk Amani Abeid Karume, amekutana na mabalozi wapya pamoja na wale wanaoondoka katika nyadhifa zao za uwakilishi.

Pichani ni Raisi Karume akizungumza na Bi Ruth Leano ambaye ni mwakilishi mpya wa UNICEF Zanzibar pamoja na Balozi mpya wa Norway nchini Bi Jorunn Maehlum ambao walitambulishwa rasmi katika Ikulu ya Zanzibar il hali walioagwa rasmi ni  Francoes Rumesi aliyemaliza muda wake wa kazi kuiwakilisha UNICEF Zanzibar na Bahar Nabil Helmy aliyemaliza nafasi yake ya Ubalozi mdogo wa Misri nchini Zanzibar.

Credits: Ramadhan Othman/Ikulu - Zanzibar via Ahmad Michuzi/Jiachie blog
 
 
Picture
Photo credit: Maggid Mjengwa
Katika historia tunajifunza kwamba katika jamii mbalimbali ardhi ndiyo ilikuwa njia kuu ya uchumi, lakini pamoja na sifa zote hizo ilizonazo, ardhi inaweza kukunufaisha kama utajua kuitumia kwa kadri sheria inavyoruhusu.

Kimsingi kwa mujibu wa sheria, ardhi inamilikiwa na serikali na wananchi wake hupewa umiliki wa muda tu kwa mujibu wa sheria kuanzia miaka 33 hadi 99 kutegemea na maombi na matumizi yaliyokusudiwa na mwombaji.

Ili kupata uhalali wa umiliki wa ardhi, mwombaji anaweza kutambulika kama mmiliki kwa kutumia sheria ya kimila ambayo inatambua umiliki wa ardhi kwa Mtanzania ambaye itadhihirika kuwa bila ya shaka alikuwa akiimiliki tangu kipindi cha kale na mamlaka za eneo husika zinatambua umiliki wake huo.

Inawezekana kabisa hati ya ardhi yako ikapotea na usijue pa kuipata tena kama zinavyoweza kupotea nyaraka nyingine katika mazingira ambayo tumezoea kuyatambua kama ni bahati mbaya.

Lakini pia ni kutokana na unyeti wake katika maisha ya wanadamu, ni rahisi ardhi kufanyiwa hujuma na mtu yeyote na mara nyingi na mtu au watu unaowaamini na wakaribu katika maisha yako ya kila siku kuhusika na upotevo wa kiwanja chako.

Awe rafiki yako kipenzi, mwanao au hata wakati mwingine mkeo au rafiki yako wa kike au kiume kuamua kuificha hati ya nyumba au kuwanja chako akiamini mwisho wa siku anaweza kuuza nyuma ya mgongo wake na kujipatia fedha kwa njia rahisi kwa sababu tu anatumia hati halisi katika kufanya biashara hiyo.

Hii inatawaliwa na dhana potofu miongoni mwa wananchi kwamba ukiwa na hati halisi hata ya kiwanja ambacho si chako kimsingi ndiyo una nguvu na mamlaka ya kufanya utakacho juu ya kiwanja au nyumba husika.

Kwa msimamo wa taratibu za kisheria kuiba au kuficha hati ya mtu mwingine haina maana au athari yoyote katika umiliki wake juu ya ardhi husika zaidi ya kusumbuana na kupotezeana muda tu na wakati mwingine hata kukusababishia kuishia jela kwa tuhuma za wizi au utapeli.

Ni vyema pindi baada ya kutambua kwamba hati yako ya nyumba au kiwanja haionekani na huna taarifa sahihi za kupatikana kwake kuanza kwa kutoa taarifa katika kituo cha polisi kilicho karibu nawe na baada ya hapo utapatiwa hati maalumu ya taarifa ya kupotelewa ambayo ndiyo itatumika kama leseni ya kutambulika kwa maelezo yako katika ofisi za ardhi husika.

Baada ya kukamilika kwa taratibu zote hizo za msingi ikiwa ni pamoja na kuijaza fomu maalumu za kisheria ambazo huandaliwa na wanasheria mbalimbali ofisi ya ardhi husika hubatilisha hati iliyopotea na kukupatia kivuli cha hati halisi ambacho kufuatia kufikishwa na kukubalika kwa taarifa hizo katika ofisi husika ya ardhi hati halisi iliyotolewa ndiyo huchukua nafasi ya hati halisi.

Kwa maana hiyo ndiyo kusema kwamba pindi baada ya kuidhinishwa kwa uhalali wa kutumia hati kivuli, hati halisi popote ilipo huwa si halali tena na yeyote ambaye ataitumia kwa namna yoyote ile iwe kuuza au kuchukulia mkopo katika benki au taasisi yoyote ya fedha atakuwa anakinzana na sheria ambayo haitasita kuchukua mkondo wake dhidi yake.

Mchakato wa kutoa taarifa na kushughulikia kupatikana kwa hati mpya unalazimika kufanyika mapema iwezekanavyo pindi baada ya kutambua upotevu wa hati husika ili kuepuka kutoa nafasi kwa aliyeichukua kwa nia mbaya kuweza kufanya taratibu za uhamisho kabla ya mhusika.

Hii ni kuhimiza umuhimu wa kuangalia na kupitia mara kwa mara hifadhi ya nyaraka majumbani kwetu ili kuepuka kuja kushtuka wakati mwizi wako ameshafanya taratibu zote muhimu zinazokubalika na zisizokubalika ilimradi tu kukupoka haki yako ya umiliki wa ardhi.

Utaratibu huu utarahisisha kujiridhisha kwako juu ya usalama wa nyaraka zako muhimu na hata kuweza kuchukua hatua za haraka baada ya kugundua upotevu wa hati husika.
 
Utaratibu wote huu mpaka kupatikana kwa hati vivuli huchukua muda mfupi na kuhusisha gharama ndogo isiyozidi 10,000 za Kitanzania bila ya kujali thamani ya ardhi au nyumba husika.

Hivyo ni vyema kwa yeyote mwenye kupotelewa na hati kukimbia katika ofisi za ardhi mapema baada ya kujiridhisha kuwa hati husika haipo mahala pake kama alivyokuwa amehifadhi awali badala ya kuhangaika kutafuta mpaka mahala kusikotafutika.

Kwa maelezo au ufafanuzi zaidi wa suala hili na mengine, tafadhali wasiliana  na mwandishi wa makala hii kupitia anwani pepe mmajaliwa@hallmarkattorneys.com au namba za simu 0655 809798 na 0786 809798 (Tz country code +255).
Credits: gazeti Mwananchi.

 
 
Ujumbe wa wabunge saba toka Tanzania ukiongozwa na Spika wa Bunge wa Tanzania Mhe. Samuel Sitta upo katika mkutano wa pamoja na wenzao wa Bunge la Uturuki pamoja na Spika wa Bunge la Uturuki Mhe. Mehmet Ali Sahin mjini Akara.

Hoja kuu ni kujadili namna ya kuimarisha mahusiano ya mihimili hii miwili ya Bunge la Uturuki na Tanzania pamoja na kuhamasisha uwekezaji katika sekta mbalimbali za maendeleo katika nchi mbili hizi.

Ziara hii ni mwitiko wa kufuatia mwaliko wa Spika wa Bunge la Uturuki kwa Spika wa Bunge la Tanzania.
 
Photo credit: Owen Mwandumbya/Bunge.
 
 
Picture
Seif Shariff Hamad - CUF
Hekaheka za maandalizi ya uchaguzi mkuu ujao zimeanza kushika kasi kwa baadhi ya viongozi wa vyama vya siasa ambapo Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF) Maalim Seif Shariff Hamad ameweka bayana nia yake ya kuwania Urais wa serikali ya Mapinduzi Zanziabar ikiwa ni miezi mitano kabla ya kinyang’anyiro hicho kufanyika.

Hii ni mara ya nne kwa Kiongozi huyo, pamoja na mwenyekiti wa CUF Taifa, Ibrahim Lipumba, ambaye naye ametangaza nia ya kugombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuwania nafasi hizo.

Akitangaza azima yake hiyo mbele ya Waandishi wa Habari mjini Dar Es Salaam, Maalim Seif amesema dhamira yake hiyo ni thabiti.

Mkutano huo ulihudhuriwa pia na Mwenyekiti wa CUF Taifa Profesa Ibrahim Lipumba ambaye ametoa rai kwa tume ya uchaguzi kisiwani Zanzibar –ZEC- kuhakikisha kuwa wananchi wanapatiwa fursa ya kujiandikisha bila kuwekewa mizengwe.

Aidha Mwenyekiti huyo wa CUF ametoa rai kwa wabunge kuhakikisha kuwa wanashiriki vema katika mchakato wa bajeti ya serikali kwa mwaka 2010 – 2011 na kuhakikisha kuwa bajeti hiyo inakuwa bora na kuwa chachu ya maendeleo na ustawi wa wananchi.

Habari kwa mujibu wa TBC

 
 
Dondoo za hizi zinatokana na mkutano wa wawakilishi wa TUCTA na Serikali uliofanyika Jumamosi iliyopita:
Picture
- Nyongeza ya kima cha chini ya sekta binafsi iliyotangazwa na Waziri Juma Kapuya imeshusha kiwango kilichotangazwa mwaka 2007.

- TUCTA haijatoa tamko kuhusu mgomo kwani inasubiri kuisha kwa siku 21 ambazo kwa mujibu wa Sheria, Waziri wa Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana anapaswa kutoa tamko la makubaliano yaliyofikiwa. Siku hizo zimeanza kuhesabiwa tangu kuisha kwa mkutano wa Mei 8.

- TUCTA ilishirikiana na wanasheria wake kupitia upya tangazo la Waziri Kapuya na kubaini kuwa halikufuata taratibu za kisheria ambazo ni pamoja na kutowashirikisha wajumbe wa bodi ya mishahara ya kisekta.

Mgaya (TUCTA) alitoa mfano kuwa kiwango cha kima cha chini cha mishahara cha sekta ya viwanda na biashara cha mwaka 2007 kilikuwa Sh 150,000, lakini katika tangazo la Waziri Kapuya kiwango hicho kimeshuka hadi Sh 80,000.

Katika tangazo hilo jipya, Serikali pia imefuta baadhi ya marupurupu ya wafanyakazi wa sekta hiyo na nyingine, ikiwa ni pamoja na posho ya nyumba, chakula, likizo na usafiri.

TUCTA iliitisha mgomo ikidai Serikali imekuwa ikipuuzia madai ya Wafanyakazi kwa muda mrefu ambayo ni pamoja na punguzo la kodi inayokatwa kwenye mishahara, kuboreshwa kwa mafao ya uzeeni yanayotolewa na mifuko ya hifadhi ya jamii na nyongeza ya kima cha chini cha mishahara katika sekta zote.

Soma zaidi habari nzima kwenye gazeti Mwananchi (bofya hapa).