Shirikisho la vyama vya wafanyakazi nchini (TUCTA), linatarajia kutoa tamko la kuhusu kugoma ama la tarehe 5 Juni 2010, baada ya kikao kinacho cha majadiliano kinachotarajiwa kufanyika Juni 4.

Hatua hiyo inafuatia Serikali kushindwa kutoa tamko la makubaliano yao ya kikao cha tatu kilichofanyika Mei 8 mwaka huu, ambapo kwa mujibu wa sheria, Waziri wa Kazi-Ajira na Maendeleo ya Vijana, anapaswa kutoa taarifa ya kikao hicho ndani ya siku 21.

Naibu Katibu Mkuu wa TUCTA, Nicholas Mgaya amesema kutokana na Serikali kushindwa kutoa taarifa yoyote ndani ya siku hizo, baraza linaloratibu mgomo litatoa tamko lake. Wafanyakazi wamekuwa kimya kutokana na kusubiri tamko la Serikali kuhusiana na kikao chao hicho, ambapo mpaka sasa Waziri ameshindwa kutoa taarifa yoyote kutokana na hali hiyo watakaa kikao hicho kwa ajili ya kujadili hatua zitakazofuatwa na wafanyakazi hao. "Tunatarajia kufanya kikao cha mwisho siku ya Ijumaa, ambacho kitatoa mwelekeo  wa wafanyakazi kufanya mgomo au la, kwa sababu tulikuwa tunasubiri tamko la makubaliano kutoka Serikalini, lakini mpaka sasa hakuna kilichofanyika badala yake waziri amekaa kimya,"alisema Mgaya.

Aliongeza kutokana na hali hiyo baraza hilo limesikitishwa na hatua hiyo, kwa  sasa wanaendelea na mikutano ya ndani kwa ajili ya kupanga utaratibu watakaotumia wakati wa kutoa tamko hilo. "Wafanyakazi ndio wanaokuza uchumi wananchi, lakini wanarudishwa nyuma na baadhi ya viongozi kwa kuwadharau na kutosikiliza matatizo yao, jambo ambalo linawafanya waingie kwenye mgogoro mkubwa namna hii na serikali," anaongeza.

Kwa mujibu wa Mgaya, mbali na tamko hilo pia, siku hiyo hiyo shirikisho hilo litatoa taarifa za kutaka kumshitaki Waziri huyo kutokana na kutangaza mishahara yenye mapungufu katika baadhi ya vipengele.

credit: Patricia Kimelemeta/Mwananchi
 


Comments

31/05/2010 16:53


Viongozi wa TUCTA wamewaangusha wafanyakazi wenzao katika mapambano na serikali kwa viongozi hao kujifanya wanasiasa.

Viongozi hao kama kweli walikuwa na nia njema ya kuongea hadi kufikia masikilizano na serikali, wasingelazimisha kufanya maandamano wakati serikali na viongozi wake walikuwa wakipokea ugeni mkubwa ambao ni nadra sana kupatikana katika nchi kama Tanzania.

Kwa ajili ya nia ya viongozi hao ya kufanya Maandamano hayo, walipata "karipio" kali kutoka kwa Mh. Rais KIkwete hapo Diamond Jubilee.

Karipio ambalo limesababisha "mtafaruku" mkubwa wa maoni, kwa kuwagawa wananchi na kumsababishia Rais wetu kulaumiwa na baadhi ya watu kwa kile alichowaambia viongozi hao wa TUCTA.

Kitendo cha viongozi wa TUCTA cha kujifanya wanasiasa, kwa maoni yangu mimi naona kimewashushia hadhi yao mbele ya wananchi wengi ambao hapo mwanzo walikuwa wakiwaunga mkono katika mapambano yao na serikali.

Kwa hiyo hata kama watafanya maandamano hayatafana kama ambavyo wao wanadhani. Wamewagawa wananchi. Watakaowaunga mkono katika maandamano yao ni wale wanaoshabikia "Upinzani" wa kisiasa, na ndiyo maana Viongozi wa Upinzani ndiyo wanaowaunga mkono.

Kwa sasa sioni sababu ya serikali kuwazuia kufanya "Maandamano" yao. Serikali iwaruhusu waandamane na hakuna kikubwa watakachokipata kama ambavyo vyama vya Upinzani wanapoandamana wasivyopata japo ushindi katika chaguzi zote. Andamaneni kwa afya zenu, wala Waziri anayehusika na Kazi asiwe na mchakato. Ukweli unabaki ni ukweli, serikali isilazimishwe kubeba mzigo isiyouweza.

This Is Black=Blackmannen

Reply



Leave a Reply