Chama cha waandishi wa Habari za Sanaa na Utamaduni Tanzania (CAJAtz) kimeshtushwa na kusikitishwa na uamuzi wa Bodi ya Biashara ya Nje (BET) wa kupiga marufuku maonyesho ya Muziki na Ngoma za Utamaduni katika Maonyesho ya Biashara ya Kimataifa yanayoendelea jijini Dar es Salaam.
Picture
photo credit: Co Broerse/flickr.com
Kupitia waraka wake uliotolewa na Utawala, BET imepiga marufuku maonyesho yote ya sanaa za Kitanzania ikiwemo ngoma, muziki na maigizo kwa madai kwamba ni kelele. Wa huohuo muziki unaosikika kwenye spika kubwa (katika viwanja hivyo) ni ule wa wasanii kutoka nje ya nchi.

CAJAtz inatambua thamani ya sanaa na Utamaduni wa Taifa hili na inaamini kwamba sehemu kama hizo ndiyo muafaka hasa katika kutangaza shughuli za sanaa na Utamaduni wetu.

Tunaamini pia kwamba katika maonesho hayo ya biashara makampuni na asasi mbalimbali huwatumia wasanii katika kufikisha ujumbe wao kwa watu mbalimbali hasa kwa kuamini katika nguvu ya sanaa. Tunashangaa leo hii kuona BET inawakataza wasanii kutumia fani zao kutoa ujumbe kwa watu licha ya kuwa makampuni na asasi hizo zimetumia pesa kuwakodi wasanii hao.

CAJAtz inaamini kwamba sanaa ni biashara hivyo kwanza ilipaswa kuachwa ili ijitangaze kupitia maonesho hayo. Pia BET inapaswa kufahamu kwamba kwa miaka yote ambayo wameilezeza kuwa na mafanikio makubwa katika maonesho hayo, sanaa hizo na ngoma vilikuwa vinatumika sana katika kusherehesha, kutoa ujumbe na kuelimisha wananchi juu ya mambo mbalimbali ya washiriki.

Kwa kitendo cha kupiga marufuku maonesho ya sanaa, BET imekosa Uzalendo wa utamaduni wetu na pia imebana ajira ya wasanii wengi walikuwa wameajiriwa na makampuni kwa ajili ya kufanya shughuli za maonesho kwenye mabanda yao.

Kwa msingi huo, sisi wadau wa masuala ya sanaa na Utamaduni hapa nchini, CAJAtz, tunalaani vikali zuio hilo ambalo halina tija na limeegemea zaidi ulimbukeni na kasumba ya watu wa kuthamini sanaa za nje na kuwatukuza wageni wachache kwa visingizio visivyo na maana.

Iweje sanaa za Kitanzania iwe kelele na hizo za magharibi iwe burudani?

Tunaiomba Serikali kupitia Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo kulishughulikia suala hili haraka iwezekanavyo. Pia tunomba BET kutafakari upya zuio hilo.

Hassan Bumbuli
Katibu Mkuu CAJAtz
credit: Beda Msimbe/Lukwangule blog
 


Comments

30/06/2010 19:14

CAJAtz,

Habari ya kuzuia burudani za Kitanzaia viwanja vya maonyesho ya Sabasaba kama ni kweli. Itakuwa ni kitu cha ajabu sana kilichobeba sifa ya "Uhujumu" wa Taifa.

Kiongozi aliyetoa amri hii tunaiomba Wizara husika imchukulie hatua kali za kumfukuza kazi na kumhoji kitu kilichomfanya kuwadharau Watanzania wote kwa kuuita "Utamaduni" wa Kitanzania ni kelele.

Kama ni hivyo, Viongozi wa BET hawapo hapo kwa manufaa ya Watanzania. Mtu huwezi kuudharau Utamaduni wako hadi kufikia kuuita ni "kelele". Kama kweli unafanya kazi yako kwa manufaa ya Watanzania huwezi kudiriki kusema ni kelele.

Sakata kama hili yafaa hata Waziri anayehusika na shughuli za Maonyesho haya atoe kauli yake. CAJAtz fuatilieni mmsikie anasemaje.

Maonyesho yapi ambayo hayaendani na miziki au ngoma za kitamaduni? Mbona nilipokuwa mtoto nilisikia marehemu Mbaraka Mwinshehe na Bendi ya Morogoro Jazz Band na Morris Nyunyusa walienda Japan kwenye Maonyesho ya EXPO-70?

Ina maana viongozi wa Tanzania katika msafara wa EXPO-70 walikuwa wanapenda makelele? Au walikuwa ni Washamba sana enzi hizo na walikuwa wanazoa takataka zote zenye kelele, Moro Jazz na Morris Nyunyusa na ngoma zake kumi?

CAJAtz tupo pamoja na ninyi kwa nguvu zote ikiwezekana hata baada ya Maonyesho haya, jambo hili lipelekeni mbele ili kupata majibu ya kuturidhisha Watanzania wote, sababu ya kudharauliwa kwa ngoma na miziki yetu kwenye Maonyesho hayo.

Kuna Watanzania wanaokaa nje ya Tanzania wamekuja kusherehekea na Watanzania wenzao katika onyesho kabambe la nyimbo za "Zamani". Leo hii mtu anakuja kusema eti ni kelele. Mimi simwelewi kama ambavyo wengine hawamwelewi mtu huyu.

It's Great To Be Black=Blackmannen

Reply
30/06/2010 23:50

Ni kweli mtu mzima hakosei bali hupitiwa kidogo lakini kwa hili BET hawajatumia busara na wamesahau kuwa Jasiri haachi asili na muacha asili ni hasidi.Kulia na kucheka zote ni kelele lakini kila kimoja kina nafasi yake na kukubalika na jamii husika.BET wao wamepewa dhamana na watanzania na si vema wakatumia dhamana hiyo kinyume na matarajio ya jamii husika.

Reply



Leave a Reply