Watu saba wamekufa papo hapo na wengine wanane kujeruhiwa katika ajali ya lori iliyotokea usiku wa kuamkia jana wilayani Handeni, Tanga. Habari zilizolifikia gazeti la Mwananchi jana zimeeleza kuwa lori hilo aina ya FUSO lililobeba abiria 15 kutoka Dar es Salaam kuelekea Moshi, mkoani Kilimanjaro, liliacha njia na kupinduka katika kijiji cha Kitumbi.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga, Liberatus Sabas alisema ajali hiyo ilitokea saa 5:00 usiku wa kuamkia jana na kuwa watu sita kati ya waliofariki ni wanaume na mmoja ni mtoto wa kike mwenye umri wa miaka mitatu. Miili ya waliokufa katika ajali hiyo imehifadhiwa katika Hospitali ya Magunga Korogwe. "Majeruhi akiwemo utingo gari hilo pia wamelazwa katika hospitali hiyo, lakini dereva wa gari hilo ametoroka, na polisi wanaendedelea kumtafuta," alisema Kamanda Sabas.

Ajali hiyo imetokea siku chache baada ya ajali nyingine iliyolihusisha lori aina ya  FUSO iliyotokea mkoani Rukwa kuua watu 5 na ile ya lori kupinduka na kusababisha vifo vya watu 15 na majeruhi 48 huko Kondoa mkoani Dodoma.
 


Comments




Leave a Reply