Picture
Ameniuliza swali msomaji mmoja wa wavuti, kuhusu kushika mimba, anasabahi vyema kisha anauliza, "...ni siku gani nzuri mwanamke akifanya mapenzi ana uhakika wa kubeba mimba 100%?"

Nilipokuwa nimeanza kujibu, nikapata wazo kutizama kama yupo yeyote aliyewahi kuandika lolote kuhusiana na hili. Na kwa bahati nzuri, nikayapata maelezo muafaka ya Dada Shally katika blogu yake ya Kona ya Afya ambapo amechanganua kwa uzuri kabisa jinsi ya kuzitambua siku za mzunguko wako wa hedhi na hatimaye kung'amua siku za kuweza kupata ujauzito na kushika mimba. Hivyo sina sababu ya kurejea maelezo ambayo tayari yanajieleza vyema.

Kwa kawaida ukishafahamu urefu wa mzunguko wa siku zako za hedhi, basi siku yoyote kati ya 10 hadi 16 ya mzunguko ni siku ambazo ni wengi hushika mimba. Sasa utazifahamuje siku hizo za kati ya 10 hadi 16 katika mzunguko wako? Kujibu swali hilo, soma maelezo ya Dada Shally.

Cha ziada katika maelezo ya Dada Shally ni kuwa msomaji, ikiwa hayajakidhi haja yako, ninakushauri ufike katika Zahanati/Kituo cha Afya au Hospitali ambayo ina mtoa huduma na/ama mtaalamu wa masuala ya uzazi ambaye atakupa maelezo zaidi baada ya kukuhoji na kupata historia yako kwa ufupi kisha atayajibu maswali yako kwa kina zaidi na kukupa ushauri kadiri ya huduma zinazopatikana ndani na nje ya nchi kulingana na suala lako na uwezo wako.

Kwa aliye na simu za kisasa au kompyuta, unaweza kupakua "app" itakayo kusaidia kurekodi na kufuatilia siku zako. Nenda www.google.com kisha andika "ovulation tracker app", pakua inayokubalika na simu yako.

Afya bora ni haki ya kila mwanadamu, na, unayo haki kuitafuta popote. Maisha yako ni jukumu lako! 


Picture
photo: tryingtoconceivetips4u.com
Nukuu ya maelezo ya Dada Shally: "Zijue siku zako za kushika mimba"

Nimeamua kuandika makala hii ili kujibu swali la moja wa mdau wa blogi hii ambaye ameuliza kwamba, anahitaji kushika mimba na je, kwa mfano mwezi huu alianza period yake tarehe 17 Juni, ni zipi siku zake za kushika mimba? Ndugu mdau kwanza kabisa nachukua nafasi hii kukuomba samahani kwa kuchelewa kujibu swali lako. Pengine ninapoandika makala hii utakuwa tayari umeshashika mimba, basi kama ni hivyo hakuna tabu bali natumaini swali lako litakuwa limewasaidia wengine ambao pengine wana tatizo kama halo. Pia umeualiza je, ukitaka mtoto wa kike ufanyeje? 

Nachukua nafasi hii kwanza kujibu swali lako la kwanza kabla sijaenda kwenye swali lako la pili. Kwani kuelewa vyema swali la kwanza kutasaidia kuelewa swali la pili pia. 

Inafaa tufahamu kuwa ili kuweza kujua ni siku zipi za mwezi mwanamke anaweza kushika mimba (to conceive) inabidi tujua kwanza kipindi ambacho mwili wa mwanamke uko tayari kushika mimba au Ovulation Period. Ovulation ni wakati ambao yai lililokua hutoka katika mirija ya ovari katika kizazi cha mwanamke na katika wakati huu uwezo wako wa kushika mimba ni mkubwa. Kwa kawaida mwanadamu huwa na mayai kadhaa katika ovari zake kwa wakati maalum wa mwenzi, ambapo yai kubwa kuliko yote huondoka na kueleka katika tumbo la uzazi kupitia mirija ya ovari. Ovulation haifuati mpangilio maalum kati ya ovari katika kila mwezi na haijulikani ni ovari gani itatoa yai kila mwezi. Wakati yai linapotoka huwa na uwezo wa kurutubishwa au kukutana na mbegu ya kiume na kuanza kutengeneza mtoto kwa muda wa masaa 12 hadi 24, kabla halijapoteza uwezo wake. Iwapo yai litafanikiwa kurutubishwa na mbegu ya kiume kwa wakati maalum na kujikita katika fuko la uzazi basi matokeo yake ni mimba. Na iwapo halitorutubisha yai hilo pamoja na kuta za kizazi huharibika na kutoka nje ya mwili kama damu ya hedhi. 

Nimetangulia kueleza haya kama utangulizi kabla ya kuzieleza siku za kushika mimba kwani kuelewa suala hilo kutatusaida kujua umuhimu wa kujua idadi ya siku zetu za mzunguko wa mwezi (Menstrual Cycle) na umuhimu wake katika kushika mimba na hata katika magonjwa ya wanawake. Ili kuelewa vyema siku hizo inatubidi tujue kitu kinachoitwa Kalenda ya Ovulation au kalenda ya kubeba mimba na pia tujua mzunguko wetu wa hedhi una siku ngapi. Mzunguko wa mwezi ni siku ya kwanza unayopata damu yako ya hedhi hadi siku kabla ya kupata tena hedhi nyingine. 

Wataalamu wanatuambia kuwa ili kujua mzunguko huo vyema inatubidi tuchunguze hedhi yetu kwa miezi isiyopungua 6. Lakini kama una haraka na huwezi kuchunguza kwa miezi 6 chunguza kwa miezi mitatu. Unaweza kufanya hivyo kwa kutumia kalenda ya kawaida na kwa kuziwekea mduara kwa kalamu siku zako za mwezi, yaani siku ya kwanza ya kupata damu ya hedhi hadi siku ya mwisho kabla ya hedhi inayofuata. Mzunguko wako wa mwezi ni siku ya kwanza ya hedhi hadi siku ya kabla ya kuanza hedhi nyingine. Kwa mfano iwapo nimepata siku zangu tarehe Pili Julai na nimepata tena siku zangu tarehe 29 Julai, mzunguko wangu ni wa siku 28. Kwa kawaida mzunguko wa siku 28 ndio mzunguko wa kawaida kwa wanawake wengi. Lakini kuna baadhi ya wanawake huwa na mzunguko wa chini ya siku 28 na wengine huwa na mzunguko wa hadi siku 35.  

Picture
Ni vipi utazijua siku zako za Ovulation 

Wakati wa Ovulation katika mzunguko wa mwezi huainishwa na luteal phase, katika mzunguko wako. Unaweza kujua muda wa Ovulation katika mzunguko wako wa mwezi kwa kutoa idadi ya siku za luteal phase. Katika kuhesabu huko utapata mzunguko mfupi na mrefu. Chukua mzunguko mfupi wa mwezi na hesabu idadi ya siku katika mzunguko huo. Toa 18 katika mzunguko huo na utapata idadi fulani. Halafu anza kuhesabu siku yako ya kwanza ya mzunguko wa hedhi katika mwezi unaofuata kwenda mbele hadi kufikia namba ulioyopata, hivyo utaweza kupata siku ambayo una uwezekano mkubwa wa kubebea mimba. 
Kwa mfano mzunguko wako mfupi ni siku 29, unatoa 18 katika 29 na unapata 11. Iwapo siku yako ya kuanza hedhi mwezi ujao ni Oktoba 3, ongeza siku 11 kuanzia siku hiyo. Hivyo siku ambayo una uwezekano mkubwa wa kubeba mimba itakuwa Oct. 14. 

Halafu chungua idadi ya siku za mzunguko wako mrefu wa hedhi. Toa siku 11 kutoka katika idadi ya siku za mzunguko huo na utapata namba fulani. Halafu tena anza kuhesabu katika mzunguko wako ujao wa hedhi kwenda mbele hadi kufikia siku ambayo una uwezekano wa kupata mimba.

Kwa mfano iwapo mzunguko wako mrefu ni siku 31, toa 11 katika mzunguko huo na utapata 20. Iwapo hedhi yako ijayo inaanza tarehe 3 Oktoba, ongeza siku 20 kuanzia siku hiyo na tarehe 23 Oktoba itakuwa siku yako ambayo una uwezekano mkubwa wa kubeba mimba. 

Kwa utaratibu huo utakuwa umepata kipindi cha kati ya Oktoba 14 hadi 23 ambacho ni siku ambazo una uwezekano mkubwa wa kubeba mimba au Ovulation window kwa kimombo. 

Ovation huweza kubadilika kidogo katika mzunguko wako wa hedhi kwa sababu Ovulation huweza kucheleweshwa na sababu mbalimbali kama vile wasiwasi au fikra nyingi, ugonjwa, lishe au kufanya mazoezi.

Vipi kipindi cha Ovulation kinaainisha ziku za kubeba mimba?
Kipindi cha kubeba mimba huanza siku 4 hadi 5 kabla ya Ovulation, na humalizika masaa 24 hadi 48 baada ya hapo hii ni kwa sababu muda wa ovulation huweza kuchelewa au kuwahi kutokana na sababu mbalimbali. Pia kwa sababu mbegu ya kiume huwa na uhai kwa siku 4 hadi 5 na yai huweza kuishi kwa masaa 24 hadi 48 baada ya kuingia katika tumbo la uzazi. Hivyo kwa kujua siku hizo humsaidia mwanamke kufahamu kipindi chake cha Ovulation kimewadia na hivyo kuweza kukukutana na mumewe au mwenza wake wakati huo ili aweze kubeba mimba. Pia kujua kipindi hiki na masuala mengineyo kama hali ya joto la mwili ilivyo wakati wa Ovulation huweza kutumika kama njia ya kuzuia mimba. Yaani kutojamiiana katika kipindi hiki huweza kumzuia mtu asipate mimba. 

Kwa kuwa kipindi cha Ovulation hakina tarehe maalum na ni siku kadhaa, katika makala ijayo nitaendelea kuzungumzia baadhi ya alama za mwili zinazosaidia kutambua ni wakati gani Ovulation imewadia. 
Daima tuzilinde afya zetu! 

[credit: kona-ya-afya.blogspot.com

 


Comments

Evans
19/11/2011 23:32

Asante sana wavuti

Reply
omega
26/11/2012 16:29

safi uchambuzi mzuri amekaa vyema

Reply
D.Ndunguru
13/01/2013 23:06

nimepeda sana somo.muendelee.

Reply

Your comment will be posted after it is approved.


Leave a Reply