Mtoa maoni Kahabi ameandika hivi katika ukurasa wa facebook,

"Wavuti.com ni kisima cha fursa kwa watanzania kuanzia habari, kazi, Scholarships na kadhalika. Nilipata kazi katika shirika la kimataifa kutokana na Tangazo kwenye tovuti hii. Pia nilipata Scholarship ya kusoma nje ya nchi kutokana na Tangazo katika tovuti hii. Kwa Mtanzania mwenye nia ya kufanikiwa katika maisha yake hatamaliza siku bila kusoma habari mpya na Matangazo katika tovuti hii. Ukijisajiri kila siku wanakutumia e mail yenye habari na fursa mpya. Ni kama vile unaletewa kazi na fursa nyingine katika mlango wa nyumba yako.

Ndugu Kahabi, shukrani kwa kutoa ushuhuda huo kuhusu wavuti.com na kwa jinsi ulivyofaidi na kuwahimiza wengine kuitumia vilivyo tovuti hii ili kupata mengi kwa faida zao na taifa lao. Ni matumaini yangu kuwa wengi zaidi watazidi kuiperuzi wavuti.com katika kurasa zake mbalimbali na kupata yatakayowafaa.

Nami nakupa pongezi kwa kufaidika na wavuti.com, ambalo ndilo lengo kuu la uwepo wake, yaani kushirikishana.
 


Comments

Lulu
12/01/2012 16:03

Naungana na mtoa mada kutoa pongezi nyingi kwa Wavuti.com. Ni blog ambayo si ya wapenda kujikweza au kujionyesha bali kwa watu wenye mtizamo wa kuona mbali. Wavuti ni shule na kioo cha kweli cha jamii. Blog nyingi huwa ukifungua unategemea kukuta picha za aina fulani au habari zinazolenga rika fulani lakini hapa ni kwa kila tabaka na rika mradi tu upende ukweli na uwazi.

Nimekunwa na jinsi ulivyoweza kuweka ile hotuba ya mbunge wa CUF. Swali ni je, kuna polisi ambao wanafungua hii blog? kama wapo je, wamemfuata mbunge kumhoji kuhusu shutma na matusi aliyombwagia mheshimiwa Sitta na baba wa Taifa??? Je, maneno yake huyo mbunge ni laini kuliko yaliyoandikwa na karamu ya Mwigamba??

Dada Subi wewe unatangulia wengine wanafuata ingawa kuna watu kama Majjid ambaye nikifungua blog yake huwa naweza kukaa muda mrefu sawa na kwako. Ila wewe ni kila baada ya masaa unatuhabarisha na kutujuza. Nimejifunza mengi tangu nilipoanza kufungua blog yako na nimefanikiwa kuwashawishi marafiki zangu kuiweka kwenye favorites zao.

Nazidi kukushukuru na kusema keep it up!!!!!!!!

Reply
12/01/2012 19:12

Ni faraja sana kuona kitu kama huu ukumbi wa wavuti unawafaidia watu. Hongera kwa kazi kubwa ufanyayo Da Subi. Sisi tunaokufahamu tangu zamani tunaelewa vizuri mchango wako, sio kwa njia ya ukumbi huu tu, bali kwa njia zingine. Mungu azidi kukubariki.

Inatakiwa wengine wafuate nyayo. Jambo moja ni kwamba kama vile wewe unavyojitolea kuendesha ukumbi huu, kutafuta taarifa na kuziweka hapa, wadau nao wawe na moyo wa kuchangia. Kama kuna mijadala, kwa mfano, yeyote mwenye jambo linaloweza kuboresha mjadala achangie.

Lakini, ukipita kwenye hizi blogu zetu, utaona mambo mengi ambayo ni kinyume. Utaona mada imeanzishwa, na halafu wanakuja wadau waitwao "anonymous" wanaandika maneno ya kuchefua na kuchafua hali ya hewa, bila mchango wa maana kwenye mada. Kwa hivi, tunaposifu na kushukuru juhudi ya wavuti, tutambue pia wajibu wetu, kwa kuzingatia mfano wa wavuti.

Napenda kurudi kwenye hoja ya mdau hapa juu, kuhusu watu kujikweza. Ningependekeza tutafakari suala hili kwa kina.

Wa-Tanzania tunaona mtu kujikweza ni jambo lisilofaa. Tunaogopa hata kujitangaza. Lakini je, inakuwaje kwamba kwenye mila za zamani za makabila yetu, kujikweza ilikuwa ni sehemu ya mila? Kwa mfano, katika utamaduni wa wa-Haya, mtu ulitegemewa kufanya mambo ya maana na kisha kujitungia majigambo. Kujigamba na wengine kukusifu katika majigambo ilikuwa ni sehemu ya utamaduni.

Hii jadi ya kufanya mambo bora na kisha kujimwagia sifa au kumwagiwa sifa ilikuwa ni sehemu ya tamaduni nyingi. Mimi ni mtafiti, na ningeweza kutoa mifano kutoka sehemu mbali mbali za Afrika, kama vile Afrika Kusini, Zimbabwe, Rwanda, Nigeria, Mali, Senegal. Kuna machapisho mengi yanayoelezea jadi za huko kote.

Kwa hivi, tutafakari ni wapi na lini sisi wa-Tanzania tuliachana na jadi hii, tukajenga dhana ya kujikweza kama ni kitu kibaya.

Nikiondoka kwenye upeo wa mambo ya mila za zamani, napenda nije kwenye dunia ya utandawazi wa leo. Dunia hii ina ushindani mkubwa sana katika nyanja mbali mbali. Huku Marekani, kwa mfano, ni utamaduni wao kuhimiza kwamba mtu ufanye vizuri katika nyanja zako, halafu unajitangaza. Vijana shuleni wanafundishwa namna ya kuandika wasifu wao. Wasifu huo huitwa "resume." Ukitafakari, utaona kuwa "resume" ni kama majigambo yale ya wahenga wetu, ila katika mazingira ya leo.

Humo hamna cha kujibaraguza. Kama ulifanya kitu cha maana, unakitangaza vilivyo. Ndio wenzetu wanavyowaandaa vijana wao katika ushindani wa utandawazi wa leo.

Nimewaona wa-Kenya huku ughaibuni na jinsi wanavyofanya tofauti na sisi wa-Tanzania. Mkenya anajitangaza, tena kwa kujiamini. Ndio maana hata Tanzania wa-Kenya wanajichukulia ajira, wakati wa-Tanzania wanaogopa kujikweza. Mkenya hajivungi.

Juzi hapo, kwa mfano, niliongea na mama mmoja m-Kenya aishiye hapa Marekani. Ni mwanataaluma, ambaye ana shahada ya udaktari. Alikuwa ananiambia kuwa amefanikiwa kuandika mradi na ambao umemletea hela zitakazomwezesha kufanya mengi nchini Kenya. Jinsi alivyokuwa ananieleza, wa-Tatnzania wangesema anajikweza. Lakini mimi kwa vile naelewa hali halisi ya Marekani, na halafu huyu mtu namfahamu kuwa ni mtaratibu tu, nilicheka kimya kimya, kwa kuwazia wa-Tanzania wangemwonaje.

Naomba nisisitize kuwa ninachosema ni kuwa watu wajibidishe katika nyanja au fani zao ili wapate mafanikio mazuri, na halafu iwe sahihi kutangaza mafanikio hayo, kwani dunia ya leo ndivyo inavyokwenda. Sisemi kuwa mtu ajitangaze mambo ya uongo ambayo hajafanya, yaani mbwembwe zisizo na msingi. Sisemi hivyo.

Kutangaza unachojua au unachoweza ni njia moja ya kuwapa walimwengu fursa ya kukugundua, na hapo wanaweza kukutafuta uwasaidie kwa hili au lile. Tufikirie upande huu pia, na tutaona kuwa hiki kinachoitwa kujikweza, kikieleweka vizuri, kwa misingi hii ninayoelezea, kina manufaa kwa wanadamu.

Reply
Kangantebe
13/01/2012 03:01

Nafurahi na watu wengine wameliona hili.

Asanteni nyote kwa kuliona na hili na kurudi kutoa shukra.
Kusema kweli hata ingekuwa mimi ningepata nguvu kuona kazi yangu inazaa matunda na watu wengine wanafaidika.

Huyu mwenye wavuti.com ni kama malaika;aliyeletwa kwetu kutuonyesha njia na mapito mema.Asante wavuti.com

Huwezi amini niliomba mwaka huu watu watambue kazi ya huyu binti na wawajulishe wengine wafaidike nayo.

Reply
13/01/2012 08:06

Ni jambo lisilopingika kuwa unapofanya jambo lolote, kupata majibu ya matokeo ya jitihada zako husaidia sana kujua kama unafanya lililo sahihi kadiri ya makusudio yako na hivyo uendelee, au unakosea wapi na hivyo urekebishe au uache kabisa.

Huwa inavunja moyo kufanya jambo na usipate matokeo, ukabaki kuwa na maswali ikiwa unalolifanya lina maana yoyote kwa wakusudiwa.

Hivi, nyote mliotoa maoni hapa mnanipa imani kubwa kuwa ninalolitanya linazaa matunda mazuri kadiri ya makusudi yangu.

Na kusudi langu kuu la kuwa na wavuti ni kushirikisha habari na taarifa mbalimbali zinazowahusu Watanzania na Tanzania katika dunia hii.

Anapopata ufadhili wa masomo mmoja kati ya Watanzania wengi, ni fahari kwangu. Anapopata ajira Mtanzania, ni furaha kwangu kuwa anapunguza idadi ya wategemezi na huenda akawasaidia wengi. Anapopata nafasi ya kuendeleza ujuzi au msaada wa fedha kwa ajili ya mradi wake, ni furaha kwangu kuwa tunasonga mbele. Tunapohabarishana yanayotokea nchini na yale yanayotokea nje ya nchi lakini yanaweza kutuathiri, inasaidia sana kujua tuenende vipi bila kuvunja sheria.

Nashukuru sana nyote mnaofika hapa kusoma, kuchangia na hata kuwahabarisha wengine kuhusu wavuti.com.

Naomba ushirikiano zaidi katika kutuma taarifa na habari mbalimbali, ili zichapishwe na kuwafikia wengi zaidi.

Heri na baraka za mwaka 2012 zionekane zaidi!

Asanteni!

Reply
alledros
14/01/2012 04:22

Kweli: kwangu Wavuti ni chai ya asubuhi! Ni kitu cha kwanza kwa kuangaza siku... Nimewashawishi wengine na wengi walipata faida mpaka kazi. Go on, ni faida kubwa kwa jamii. Kwako ni kazi ngumu nakushangaa kwani unaweza kujinyima mengi hasa 'time' bila faida, bila kupata fedha1 ni mfano kwa wengi tunaotafuta faida kwa kila tunachofanya na hatujui kujitolea au kuwashiriksha wenzetu tulichonacho! Wengi tunatawaliwa na uchu, wivu na choyo! Mungu awe nawe.

Reply



Leave a Reply