Gazeti la Mwananchi la leo, Jumanne, Januari 31, 2012 limeandika habari zenye kichwa cha habari – JK abariki posho mpya za Wabunge: Kila mmoja kulipwa sh 330,000 kwa siku. 

Habari hizi siyo za kweli na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais inataka kutoa ufafanuzi ufuatao:  

Maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete kuhusu suala hili yako wazi kabisa na hakuna mahali ambako Rais Kikwete amebariki posho hizi. 

Maelekezo ya Mheshimiwa Rais kuhusu suala hili ni kama ifuatavyo:

Kwanza, Mheshimiwa Rais Kikwete anakubali haja ya kuangalia upya posho kwa Wabunge lakini amewataka  wabunge kutumia hekima na busara katika kulitafakari suala hili. 

Pili, Mheshimiwa Rais Kikwete amewataka Wabunge kutumia Kikao cha sasa cha Bunge kulizungumza upya suala hilo.
Mwisho.

Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu.
Dar es Salaam

31 Januari, 2012 

(source)
 


Comments

Pessimism
31/01/2012 07:16

Nikiwa Mtanzania nashindwa kujua kwa nini taarifa hizi za kutatanisha kuhusu Mh,Rais kubariki au kutobariki posho za wabunge tunazipata kupitia WAVUTI.
Na nashindwa kujua kama Wavuti ni mtandao madhubuti wenye kutoa habari sahihi na kwa wakati kwa umma.
Hili nalisema kwa sababu Wavuti wametoa taarifa ya Mh.Waziri mkuu akiliarifu Bunge kuwa rais amebariki posho hizo.Habari iliyopo hapo chini.
Tena tunapata taarifa kutoka kurugenzi ya mawasiliano Ikulu kuwa Mh rais hajabariki posho hizo.Huu ni uhuni wa Wavuti mnaoufanya wa kuchapisha habari bila kufahamu ukweli wake.Sasa tuwaeleweje na tuamini lipi??

Reply
31/01/2012 07:38

Hivi huwa unasoma mwisho wa habari palikoandikwa "via..." au "source" au "chanzo cha taarifa..." kweli? au kwa kuwa ni Pessimist basi umeathirika na maana ya jina lako kwa hivyo huwezi kujua maana ya kuwepo maneno hayo mwishoni mwa habari? Kweli wewe una-pessimism maana yote uliyoandika hapo ni pessimistic ideas, jina lako jibu tosha.

Reply
Kombukela
01/02/2012 00:28

Subi, umenena vema, manake jamaa nashindwa kumuelewa kabisa na nina wasiwasi na umakini wake katika kusoma hizi habari na kuzifanyia tathmini.

Ng'wanamvanga
31/01/2012 07:57

Kwa uelewa wangu (unaweza kuwa mdogo), mwendesha wavuti anaitumia kama blogu kwa maana kwamba si lazima kila anachochapisha awe amekitengeneza yeye. Blogu, tofauti na magazeti-mtandao, zinazuruhusu kuchapisha habari toka kwa bloga wengine au magazeti mradi tu mwendeshaji wake anaainisha chanzo cha habari.

Pessimism, pengine hakuwa anafahamu hilo... lakini ndio kujifunza; mara nyingine unapotembelea wavuti kuwa makini kuangalia chanzo cha habari, kisha ujiongeze kama unafaa kuamini hiyo habari au la!!

Reply
31/01/2012 08:05

Asante sana Ng'wanamvanga kwa maelezo yako, sahihi na ninayaafiki. Wewe unaielewa wavuti vilivyo ndugu yangu. Pengine hata sikuhitaji kulipuka kama nilivyofanya hapo juu, ninapaswa niendelee kufahamu kuwa wapo wanaoifahamu wavuti na wapo wageni, basi, nijifunze kuchukuliana na wote!

Asante Ng'wana!

Kombukela
01/02/2012 00:25

Ndugu ni vema ukatambua kuwa Wavuti imetoa taarifa mbili kutoka vyanzo viwili tofauti na zinazokinzana. Kama ni mfuatiliaji hizi habari hazipo wavuti tu zipo pia katika magazeti mengi ya Tanzania. Kwa hiyo kusema Wavuti ni wahuni hutendi haki, ni juu ya wewe kuchambua na kuelewa kuwa wanaokinzana ni hawa watendaji wa serikali yetu ambapo kila mmoja anasema lake.

Reply
Brian
31/01/2012 12:30

Too much contradictions naamin sasa serikalin/Ikulu kuna tatizo kubwa sana uongoz/Management, kwa sababu zifutazo;
-Pinda alisema hivi karibun wabunge wanamajukumu mengi mpaka kufika mwisho wa mwezi wanabakia na madeni.
-Ikulu haijawahi kukanusha pamoja na kelele zoote zilizopigwa na viongoz wa dini,wanasiasa,na wanachi kwa ujumla.
-tulicho ambulia ni tofauti za katibu wa bunge na spika wa bunge.
-Nauliza swali ikulu ina macho tu ya kusoma magazeti mahiri kama Mwanachi na The Citizen tu HAINA MASIKIO YA KUSIKIA VILIO VYA SIKU CHUNGU MZIMA?
-Naishauri Serikali kuwa DEFINE-STANDING ORDER inachukiza sana IKULU/SERIKALI kutoeleweka wala sio kupambana na magazeti,toeni tamko kuwa POSHO za wabunge ni ngapi?
-Swali jingine kama ikibainika POSHO 200000 je Tutaendelea kumwamini nani kati ya IKULU na Magazeti?

Reply
pessimism
31/01/2012 23:10

Asante wewe ndiye umenielewa mantiki ya ujumbe wangu hapo juu.
Wachangiaji wa mwanzo tushirikiane kwa hili" hivi inawezekana chanzo hiki cha habari kikatoa habari mbili kwa wakati huku zikiwa zinakinzana? hiyo ndiyo dhima ya Wavuti? dhana ya kunukirisha na kunakirisha habari zisizo za uhakika kutoka blogi nyingine ndiyo dhima ya Wavuti????
Kwa upande mwingine Mr Buriani upo sahihi kabisa.Yani serikali yetu ilisha kufa.Tunaongozwa na vivuri kwani kila jambo linafanyika kihunihuni tu.

Reply
Mnoko Makini
01/02/2012 01:37

Pessimism-Nadhani sasa umeelewa.Tatizo si watoa habari(Wavuti na magazeti).Tatizo kubwa hapo ni hao ambao habari zinawahusu(Ofisi ya bunge,Ofisi ya waziri mkuu na Ikulu)
1.Mkanganyiko wa posho za wabunge haukuanza leo-Kumbuka katibu wa bunge alitangaza posho zimepanda - WITHIN HOURS-Spika akakanusha.
2.Waziri mkuu alithibitsha kwamba Rais kapitisha posho,within hours tu Rais kupitia kurugenzi ya ikulu ikakanusha.
SASA KWA SONGOMBINGO HILI,KULAUMU VYOMBO VYA HABARI KAMA WAVUTI NA MAGAZETI NI KUWAONEA TU.

01/02/2012 01:59

@Pessimism, tafadhali hebu msome Prof. Masangu kwenye ujumbe wake huu
http://matondo.blogspot.com/2012/02/hizi-posho-za-wabunge-mbona-kasheshe.html
kuhusiana na habari hii hii ya "posho" na "matamko" ya Ikulu, Bunge, Waziri, Wabunge n.k, pengine itakusaidia.

----------- NINA NUKUU -----------

(1) Spika anasema hata hizo walizoongezewa Bado Hazitoshi

(2) Naibu Spika alishawahi sema kuwa watajadili jinsi ya kuzifuta.

(3) J.K. Aligoma kuzibariki posho hizi.

(4) Jana ikaripotiwa kuwa J.K. Amezibariki Posho Hizo

(5). Ikulu mara moja imekana kwamba J.K hajabariki posho.

(6). Waziri wa fedha naye hajui kitu kuhusu hizi posho.

(7) CCM nao wakaonyesha wasiwasi wao kuhusu hizi posho.

(6). Hii mbona kasheshe? Ni nani aliyeidhinisha kupandishwa kwa posho hizi? Nini kinaendelea katika sakata hili? Ni sarakasi, mazingaombwe ama siasa ???

--------- MWISHO WA KUNUKUU -----------

Ukibofya linki ya post ya Prof. Matondo niliyoitoa hapo juu utaona maneno yaliyokolezewa wino kila mwisho wa sentensi, ukiyabofya (click) moja moja yatakupeleka kwenye vyanzo mbalimbali vya habari hizo.

SHUKRAN

Asanteni nyote kwa kuchangia maoni kuhusu "kizungumkuti" hiki. Kweli hii nchi tunakorogwa na kuchanganywa vilivyo, mtu "usipochanganya na zako" ni rahisi sana kuachwa njia panda.

Nimesoma kwenye makundi pepe mengine huko mtandaoni taarifa zinazosema si lolote si chochote, Wabunge wamekwishaanza kupokea posho hiyo ya Tsh. 200K, kazi ni kwako kumbana Mbunge wako akuthibitishie ukweli au akukanushie uongo huo!

Reply



Leave a Reply