Wataalam wa masuala ya masoko wanasema biashara haitaji
kutumia mamilioni ya fedha katika kujitangaza bali kampeni ndogo tu ambayo
itagusa hisia za watu wengi kwa wakati mmoja. Huenda wakati TSN wakifanya hiki
hawakutegemea muitikio wa watu utakuwa chanya kiasi hiki lakini ndivyo
ilivyotokea.
![]() |
Ahmed Albaity |
Kwa muda wa takribani miaka 10 kijana Ahmed Albaity amekuwa
mgonjwa mara baada ya kupooza sehemu kubwa ya viungo vya mwili wake wakati
akiwa katika bwawa la kuogelea. Picha za Ahmed ambaye ni kijana mdogo mwenye
sura ya kuvutia zilisambazwa na ndugu zake ambao wamekuwa wakimuombea msaada wa
matibabu na kupelekea maelfu ya watumiaji wa mitandao ya kijamii hasa Facebook
na Instagram kuguswa na kuanza kuchangishana.
![]() |
Ujumbe wa Ahmed kuhusu matumaini mapya ya matibabu |
Wiki chache zilizopita Ahmed alisambaza ujumbe kupitia Whatsapp kuhusu
matumaini mapya ya matibabu ambayo yanaweza kuumaliza ugonjwa wake na kuwaomba
msaada wasamalia wema ili aweze kufikisha kiasi cha $50,000 (dola elfu hamsini
za Kimarekani) ambazo kwa sasa zina wastani wa kama Sh 110,000,000.
Ujumbe huu unaotia matumaini uliwashawishi watu wengi ambao
wamekuwa wakifuatilia maendeleo ya Ahmed kuanzisha harambee ya kuchangia
matibabu ambapo mmoja ya marafiki zake walilileta suala hili katika mtandao wa
Twitter ambako wengi walikuwa hawamfahamu Ahmed lakini baada ya kusoma ujumbe
huo waliguswa na kuanza kuusambaza na hashtag ya #AhmedAamke kuanzishwa ili
kusaidia kueneza ujumbe.
Watanzania walioko Twitter kwa muda mrefu wamekuwa na sifa
ya kufanya michango ya kijamii na michango ya pole kwa wale waliopata matatizo
ambapo itakumbukwa namna walivyoweza kuchangia madawati zaidi ya 200 kwa shule
za msingi Mjimwema ya Kigamboni na shule ya Msinune Bagamoyo pia wakiendesha
mchango wa Catheter zilizosambazwa katika hospitali za Dar es Salaam na
Morogoro, misaada kwa waathirika wa mafuriko na hata rambirambi pale mmoja
anapopatwa matatizo.
Kusambaa kwa hashtag ya #AhmedAamke ilipelekea baadhi ya
watumiaji wa Twitter kuanza kuyaomba makampuni yaliyopo kwenye mtandao huo
kuchangia ambapo mengi yalitia jicho la upofu huku baadhi yakitoa majibu ambayo
yalipelekea hasira kwa waliosoma.
Ni katika wakati huu ambapo TSN Supermarket ambayo ilikuwa
haina muda mrefu tangu ijiunge Twitter ilitoa ahadi ya kuchangia kiasi cha Sh
2,200,000 (milioni mbili na laki mbili) ambazo kwa sasa ni sawa na $1000 (dola
elfu moja za Kimarekani).
Tumeguswa na tatizo la Ahmed, tunaungana na wote kufanikisha safari ya matibabu kwa kuchanga 2,200,000/= #AhmedAamke pic.twitter.com/iJ50kbgh8w— TSN Supermarket (@TSNsupermarket) March 8, 2016
Pengine TSN walifanya hivi wakiwa kama mmoja ya
Watanzania walioguswa lakini kilichotokea huenda kiliwashangaza hata wamiliki
wake. Saa moja baada ya tweet ya kutoa
ahadi ya mchango TSN ilijikuta ikitajwa na zaidi ya watu 1,000 huku tweet yake
ikipata Retweets zaidi ya 100. Wakati ikitoa ahadi hii ilikuwa na wafuasi 11 tu
lakini baada ya masaa 12 wafuasi wake walipanda hadi kufikia 300 na mpaka
tunaandika hii idadi ilikuwa inaongezeka. Kingine cha kufurahisha ni namna watu
wengi walivyoahidi kuanza kununua bidhaa katika Supermarket za TSN huku baadhi
wakipiga selfie wakiwa ndani ya supermarket hizo masaa machache baadae.
![]() |
Michael Mlingwa mmoja ya wapiga picha maarufu jijini akionyeshwa kuguswa |
![]() |
Mchekeshaji Masanja Mkandamizaji akiwashawishi mashabiki wake kuifuata TSN |
![]() |
Habari njema, mteja mpya wa TSN |
Hii inaweza kuwa fundisho kwa makampuni mengine kuwa yanatakiwa kuitumia mitandao ya kijamii kama wanajamii badala ya kuwa kama robot wanaotangaza biashara zao. Unapokuwa sehemu ya suluhisho la matatizo ya wanajamii wanaokuzunguka bila kuombwa unatengeneza ufuasi wa kudumu “brand loyalty” kwa biashara yako.Meneja Mahusiano na Masoko TSN, Gladness akimkabidhi @OnsideJamil hundi ya mchango wa matibabu ya Ahmed #AhmedAamke pic.twitter.com/nsLHuz8459— TSN Supermarket (@TSNsupermarket) March 15, 2016
Kufahamu kwa undani kilichomkuta Ahmed hadi kufikia hali hii tazama video hii